• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 5:22 PM
Atupwa ndani wenzake wakiuawa na umati

Atupwa ndani wenzake wakiuawa na umati

Na RICHARD MUNGUTI

JAMBAZI  mwenye umri wa miaka 19 aliyejiponya nafsi yake kwa kuruka ukuta na kuingia ndani ya nyumba moja mtaani Lang’ata huku akiwahepa wananchi waliokuwa na hasira wasimle mzimamzima alisukumwa jela miaka sita kwa wizi wa mabavu.

James Okello ambaye wenzake wawili waliuawa na kuteketetezwa pamoja na pikipiki waliyokuwa wanaiendesha na kuchomoka mbio baada ya kutekeleza uhalimu alilia kwa sauti kortini alipoelezwa na hakimu matukio ya siku hiyo Oktoba 11 2020.

Hakimu mkuu Bw Abdul Lorot alimsukuma jela mnamo Jumatano na kumsihi “ajihoji akiwa gerezani kama atabadilika ama ataendelea na maisha ya uhalifu aliomweleza haulipi, hauna faida.”

Okello na washukiwa wengine wawili walimvamia Bi Rose Nduku Kioko na kumwamuru awape simu yake ya kiunga mbali kwenye barabara ya Kitengela iliyoko mtaani Langata, mnamo Oktoba 11, 2020

Bi Kioko alizuiliwa na mwendashaji bodaboda aliyekuwa amewabeba majambazi wawili waliomwamuru awape simu yake ya kiunga mbali la sivyo atajuta maisha yake yote.

Majambazi hao walikuwa Okello na watu wengine wawili waliokuwa wanasafiria kwa boda boda.

Harufu mbaya

Wakati Rose alinyoosha mkono kutoa simu ndani ya mkoba wake chake mmoja wa majambazi hao alichomoa kisu na kumtaka afanye hima la sivyo wamtoboe tumbo machengelele yake yatapakae na kumwaga “kinyesi chake chenye harufu mbaya.”

Rose alidungwa kisu pajani na kwenye tumbo kisha akapiga kamsa kisha mabawabu waliokuwa wanalinda majumba mtaani humo wakakimbia kumwokoa.

Bawabu mmoja alimtandika rungu mmoja wa washambulizi hao wa Rose kisha akamwokoa Rose ambaye tayari anatokwa na damu tumboni na pajani.

Kizaazaa kiliponoga Okello alipata fursha kisha akatoroka na kukwea ukuta na kuingia ndani ya nyumba moja kuponya nafsi yake.

Lakini hakuwa na bahati wananchi walimchomoa hapo na kumtwanga barabara kabla ya kuokolewa na polisi.

Akimuhukumu hakimu alisema ,“mshtakiwa ni mvulana mwenye umri wa miaka 19 tu. Wenzake wawili waliuawa na umati uliokuwa na gadhabu.Natumaini atajirekebisha tabia akiwa gerezani.”

Bw Lorot aliendelea kusema akimuhuku, “Uhalifu uliotekeleza ni mbaya. Ulimdunga mlalamishi tumbo na tako kwa kisu. Kweli ulihatarisha maisha yake. Kifungo cha miaka sita kitakuwa funzo kwako na kwa majambazi wengine.”

Mshtakiwa alilidodokwa na machozi hakimu alipomkumbusha jinsi alitoroka kwa mwendo wa kasi baada ya kukwepa kifo kwa sekunde chache.

Okello aliomba msamaha na wakati huo huo akamshukuru Mungu alimponya na hamaki ya wakazi wa Langata waliokuwa wanalia wamwage damu yake vile alimwaga ya Rose.

Mmoja wa majambazi wenzake alifungiwa kwenye pikipiki waliyokuwa wanaendesha wakitekeleza uhalifu huo kisha akachomwa moto pamoja na boda boda yake aliyokuwa anatumia kuwatorosha wahalifu hao.

Akimlilia hakimu amwonee huruma, Okello alidai alikuwa ametimuliwa kwa nyumba na landlodi na aliingilia uhalifu kusaka pesa za kulipia nyumba.

Hakimu alimweleza , “Uhalifu haulipi. Songa na miaka sita jela.”

You can share this post!

Waititu kupimwa corona kabla ya kushtakiwa

Jinsi ya kujikinga dhidi ya kansa ya mapafu