• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 10:55 AM
Afueni kwa wakulima wa Laikipia mradi wa uchimbaji wa mabwawa ukianza

Afueni kwa wakulima wa Laikipia mradi wa uchimbaji wa mabwawa ukianza

Na SAMMY WAWERU

Zaidi ya wakulima 500 Laikipia wanatarajia kunufaika kufuatia mradi wa uchimbaji wa mabwawa ya kuvuna maji kupitia ufadhili wa serikali ya kaunti hiyo.

Kwenye mahojiano ya kipekee na Taifa Leo, Waziri wa Maji, Mazingira na Raslimalihai, Laikipia, Bw Njenga Kahiro amesema shughuli za uchimbaji wa mabwawa hayo zinatarajiwa kuanza kabla ya mwezi Februari 2021.

Amesema mradi huo wa kufanikisha uvunaji maji unalenga kupiga jeki wakulima Laikipia na kuimarisha sekta ya kilimo.

“Tunataka kuinua wakulima ili waendelee kubuni nafasi za ajira,” Bw Kahiro akasema.

Alidokeza kwamba bwawa moja linatarajiwa kugharimu kima cha Sh300, 000.

“Mradi huu utaendeshwa katika wadi mbalimbali Laikipia, na kwa sasa tumelenga wakulima 500. Tunapania kuchimbia kila mmoja bwawa linalositiri lita milioni 2 za maji,” Waziri huyo akaelezea, akisema hatua hiyo itasaidia kuangazia uhaba na ukosefu wa maji Laikipia.

Kaunti ya Laikipia ni kati ya kaunti kame nchini. Serikali ya kaunti hiyo imekuwa ikifanya ziara kwa wakulima wanaofanya kilimo cha kipekee.

Baadhi ya wakulima wamekumbatia mfumo wa kuvuna maji kwa mabawa na pia kwa kutumia matenki, huku wakitumia mifereji kunyunyizia mashamba na mimea maji.

Licha ya mahangaiko ya maji, Kaunti ya Laikipia ni miongoni mwa wazalishaji wa mimea inayochukua muda mfupi kama vile nyanya, vitunguu, viazi, kati ya mingineyo.

You can share this post!

Wamiliki wa mikahawa walia kuponzwa na corona

Mvua kubwa Lamu yaharibu barabara