• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 11:42 PM
Je, chama cha wilibaro kitasajiliwa?

Je, chama cha wilibaro kitasajiliwa?

Na LEONARD ONYANGO

WANASIASA wamekimbia katika afisi ya Msajili wa Vyama vya Kisiasa kujaribu kusajili vyama vilivyo na nembo ya wilibaro.

Msajili wa vyama kisiasa Anne Nderitu Jumatano alithibitisha kuwa afisi yake imepokea maombi kadhaa kutoka kwa watu wanaotaka kutumia wilibaro kama nembo ya vyama vyao.

Wilibaro zimekuwa zikihusishwa na Naibu wa Rais William Ruto hivi karibuni kwa vile ni miongoni mwa vifaa alivyokuwa anavyokabidhi vijana wajasiriamali kila mwezi.

Bi Nderitu, hata hivyo, aliambia Taifa Leo kuwa afisi yake inaendelea kukagua maombi hayo. “Kwa kawaida, tutahifadhi nembo hiyo kwa ajili ya mtu aliyetuma ombi wa kwanza,” akasema.

Ni kawaida kwa watu kukimbilia kutuma maombi kusajili jina au neno ambalo ni maarufu kwenye ulingo wa kisiasa.

Kwa mfano, baada ya upande wa ‘hapana’ – uliowakilishwa na chungwa – kushinda kura ya maamuzi ambapo Wakenya walikataa rasimu ya katiba 2005, wakili Mugambi Imanyara alisajili chama cha chungwa (ODM).

Baadaye alikikabidhi kwa kiongozi wa ODM Raila Odinga uchaguzi mkuu wa 2007 ulipokaribia na Imanyara akawa katibu wa masuala ya sheria wa chama hicho, wadhifa alioshikilia hadi 2011.

Hivi majuzi, ilifichuka kwamba Msajili wa Vyama vya Kisiasa alikataa kusajili ‘Hustler’ kuwa chama cha kisiasa kwa msingi kuwa “kinaendeleza ubaguzi kinyume na Sheria ya Vyama vya Kisiasa ya 2011”.

Imedaiwa kaulimbiu ya ‘Hustler’ ambayo hutumiwa na Dkt Ruto inaweza kusbabisha mgawanyiko kati ya maskini na matajiri nchini.

Wapinzani wa Dkt Ruto, wakiongozwa na Bw Odinga, wamekuwa wakishutumu Dkt Ruto kwa ‘kuwahadaa vijana kwa kuwapa wilibaro ambayo imepitwa na wakati’.

Lakini Naibu wa Rais anashikilia kuwa wilibaro ni muhimu kwa wafanyabiashara wadogo wasiomudu gharama ya kukodisha maeneo ya kuuzia bidhaa zao.

Kando na ‘Hustler’, Afisi ya Msajili wa Vyama vya Kisiasa ilitupilia mbali pia ombi la kutaka kusajili Mpango wa Maridhiano (BBI) kuwa chama cha kisiasa hivi majuzi.

Watu wasiojulikana walijaribu kusajili BBI baada ya baadhi ya wanasiasa kupendekeza kiwe chama kitakachojumuisha wanasiasa wanaounga mwafaka baina ya Rais Kenyatta na Bw Odinga.

Miezi mitatu iliyopita, Bi Nderitu, alikataa maombi ya kutaka kusajili pia Jubilee Asili kuwa chama cha kisiasa.

Maombi ya kutaka kusajili chama cha Jubilee Asili yalimiminika baada ya Naibu wa Rais Ruto mnamo Juni, mwaka huu, kuzindua afisi mbadala yenye jina Jubilee Asili Centre katika mtaa wa Kilimani jijini Nairobi na kuzua tetesi kuwa huenda alitaka kuunda chama kipya.

Wakati wa uzinduzi huo, Naibu wa Rais Ruto alizindua kaulimbiu mpya ya “Sote Pamoja” badala ya “Tuko Pamoja” inayotumiwa na chama cha Jubilee.

Wakati huo, Bi Nderitu aliambia Taifa Leo kuwa alikataa kusajili Jubilee Asili kuwa chama cha kisiasa kwa sababu jina hilo linakiuka Sheria ya Vyama vya Kisiasa ambayo inataka jina la chama kinachopendekezwa lisifanane au kukaribina na chama kilichopo.

Kifungu cha 8(c) cha Sheria ya Vyama vya Kisiasa kinaruhusu Msajili wa Vyama vya Kisiasa kukataa ombi la kusajili chama ikiwa jina lina matusi na linafanana au kukaribiana na chama ambacho tayari kimesajiliwa.

Dkt Ruto amekuwa akijiita ‘hustler’ (mlala hoi) kwa lengo la kujitafutia uungwaji mkono miongoni mwa Wakenya maskini huku akijiandaa kuwania urais 2022.

You can share this post!

Mihadarati ya Sh70,000 yanaswa Nakuru

Sitaomba msamaha, Magoha awaambia wakosoaji