• Nairobi
  • Last Updated April 18th, 2024 9:15 PM
Huenda baadhi ya watahiniwa wakakosa mitihani ya KCPE, KCSE

Huenda baadhi ya watahiniwa wakakosa mitihani ya KCPE, KCSE

Na GEORGE ODIWUOR

WATAHINIWA wa mtihani wa Darasa la Nane (KCPE) na Kidato cha Nne (KCSE) katika shule za kibinafsi ambazo zimefungwa na wamiliki kutokana na makali ya virusi vya corona huenda wakakosa kufanya mitihani hiyo ya kitaifa.

Hii ni baada ya Wizara ya Elimu kusisitiza kuwa watahiniwa waliohamia katika shule za umma watalazimika kurudi katika shule zao za awali wakati wa kufanya mtihani.

Waziri wa Elimu, Profesa George Magoha amesema kuwa, serikali imeruhusu wanafunzi kutoka shule za kibinafsi kuhamia katika shule za umma kufuatia janga la virusi vya corona.Waziri Magoha, hata hivyo, alisema watahiniwa watalazimika kurejea katika shule zao ambapo walijisajili kufanyia mtihani wa KCPE na KCSE.

Ripoti zinaonyesha kuwa zaidi ya shule 130 za kibinafsi zimefungwa kufuatia makali ya janga la virusi vya corona.

Kulingana na Chama cha Wamiliki wa Shule za Kibinafsi (Kepsa) shule hizo huenda zikakosa kufunguliwa Januari 4, mwaka ujao.Hiyo inamaanisha kuwa, wanafunzi waliojisajili katika shule hizo kwa ajili ya KCPE na KCSE huenda wakakosa kufanya mtihani huo.

“Kuna wazazi ambao walipoteza ajira au biashara zao na watoto wao walikuwa wanasomea katika shule za kibinafsi na hawawezi kulipa karo. Mitihani imetayarishwa na hatuna muda wa kubadilisha shule ambapo wanafunzi watafanyia mitihani yao.”

Prof Magohaa lisema kuwa, serikali itatoa uamuzi wake baadaye kuhusiana na hatima ya watahiniwa wa shule za kibinafsi ambazo zitakosa kufunguliwa.

Waziri alisema kuwa kuruhusu wanafunzi wa shule za kibinafsi kujiunga na shule za umma ni miongoni mwa mikakati iliyowekwa na serikali kuhakikisha kuwa watoto wote wanarejea shuleni Januari.

You can share this post!

WANDERI KAMAU: Ulaya irejeshe mali ya Afrika ambayo...

Hofu ya maafa mgomo ukichacha