• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 2:07 PM
Wakuu wa Kenya Power walala ndani

Wakuu wa Kenya Power walala ndani

Na Richard Munguti

MKURUGENZI mkuu wa kampuni ya kusambaza nguvu za umeme nchini Kenya Power & Lighting (KPLC) DkT Ken Tarus , alishtakiwa Jumatatu pamoja na washukiwa wengine 23 akiwemo nyanya mwenye umri wa miaka 70 kwa kununua transfoma duni zilizopelekea kampuni hiyo kupoteza mamilioni ya pesa.

Na wakati uo huo hakimu mkuu mahakama ya kuamua kesi za ufisadi Bw Douglas Ogoti aliombwa na Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma (DPP) atoe kibali cha kumkamata nyanya huyo Bi Grace Wanjira Mungai , mwanawe John Antony Mungai na wafanyakazi wawili wa KPLC waliosemekana wamejificha na kuzima simu.

“Naomba hii mahakama iamuru Bi Grace Wanjira, mwanawe Antony, wahandisi Daniel Ochieng Muga na Bernard Githui Muturi wakamatwe. Wamejificha na kuzima simu. Polisi hawakuweza kuwafikia. Yaaminika wamejificha kabisa,” naibu mkuu wa DPP Bi Jacinta Nyamosi anayesaidiwa na viongozi wa mashtaka 12 alirai.

Afisi ya DPP kupitia kwa Bi Nyamosi ilipinga washtakiwa wote wakiachiliwa kwa dhamana akisema “watavuruga mashahidi na kusambaratisha haki ikitekelezwa.”

Washtakiwa walikanusha mashtaka ya ubadhirifu wa pesa za umma , matumizi mabaya ya mamlaka, kufanikisha utendaji wa uhalifu wa kuruhusu kampuni ya Muwa Enterprises Trading Company Limited.

Mahakama ilifahamishwa washtakiwa walisababisha KPLC kupoteza zaidi ya Sh700milioni kwa ununuzi wa bidhaa duni na utoaji huduma ghushi.

Walioshtakiwa ni Dkt Tarus, aliyekuwa kinara wa KPLC Dkt Ben K Chumo, meneja wakuu wa KPLC K P Mungai, Beatrice Maeso, Joshua Mutua, Abubakar Swaleh, Samuel Ndirangu, Stanley Mutwiri, Benson Muriithi, Peter Mwicigi, John Ombui, wamiliki wa kampuni ya Muwa Enterprises Co.Ltd-James Njenga Mungai , mkewe Wanjira na mwanao Antony aliyedaiwa na wakili Prof Tom Ojienda aliandamana na mama yake (wanjira) kupokea matibabu mjini London Uingereza. Kampuni ya Muwa Enterprises Co.Ltd ilishtakiwa.

Washtakiwa walikabiliwa na mashtaka ya kuruhusu kampuni ya Muwa kununua transfoma feki zinazosababisha kutoweka kwa nguvu za umeme nchini kati ya Aprili 2012 na Juni 2018.

Wafanyakazi wengine wa KPLC Wahandisi Everlyn Pauline Omondi, Harun Karisa, Daniel Tare , Noah Ogano Omondi,John Mwangi Njehia, James Muriuki, Muga , Dkt Tarus na Muturi walishtakiwa kwa ufujaji wa Sh159, 195,364 kupitia ununuzi wa bidhaa feki.

Mawakili Kirathe Wandugi, Prof Ojienda na Ken Nyaundi walipinga vibali vya kuwatia nguvuni washukiwa wanne.

“ Antony amempeleka mama yake Wanjira hospitali mjini London . Mumewe Bw James Njenga Mungai amefika kortini kujibu mashtaka kwa niaba yake na kwa niaba ya kampuni yao-Muwa-Akikamilisha kupokea matibabu nyanya huyo mwenye umri wa miaka 70 atarudi nchini. Bila shaka atafika kortini kujibu mashtaka,” alisema Prof Ojienda.

Mahakama iliombwa iwaachilie washukiwa kwa dhamana lakini afisi ya DPP ikapinga ikisema washtakiwa watavuruga ushahidi na utekelezaji wa haki. Washukiwa waliwekwa rumande mahakama ikiandaa uamuzi wa ombi lao la dhamana.

Mhandisi Jared Omondi Otieno ameteuliwa kuwa mkurugenzi mkuu mwandamizi wa kampuni ya Kenya Power & Lighting (KPLC).

Bw Otieno anatwaa mahala pa Dkt Ken Tarus aliyeshtakiwa kuwa ufujaji wa mali ya umma na usimamizi mbaya uliopelekea KPLC kupoteza zaidi ya Sh700milioni katika ununuzi wa trnasfoma feki.

Otieno aliteuliwa na Waziri wa Kawi Charles Keter baada ya misururu ya mikutano baada ya kushtakiwa kwa wakuu 21

You can share this post!

Raila akosa saizi yake

Niligonga ng’ombe wala si kuua mwanamke ajalini...

adminleo