• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 11:42 PM
Babu Owino na wenzake watisha kuandamana Kampala kumnusuru Bobi Wine

Babu Owino na wenzake watisha kuandamana Kampala kumnusuru Bobi Wine

Na CHARLES WASONGA

MUUNGANO wa Wabunge Vijana (KYPC) kitaandaa maandamano jijini Kampala Uganda Jumatatu na kuvuruga shughuli katika ubalozi wa nchi hiyo humu nchini kupinga kuzuiliwa kwa Mbunge wa Kyandodo Mashariki Robert Kyagulanyi almaarufu Bobi Wine.

Wakilaani kukamatwa kwa mbunge huyo, maarufu kama Bobi Wine wabunge Babu Owino (Embakasi Mashariki), Fred Okello (Nyando) na Gideon Keter (Mbunge Maalum) waliukosoa utawala wa Rais Yoweri Museveni kwa kunyanyasa na kukandamiza viongozi vijana.

“Kitendo cha kukamatwa, kuzuiliwa na kuteswa kwa mwenzetu ni kielelezo cha ukiukaji wa haki za kibinadamu. Dhuluma dhidi ya kiongozi yeyote kijana ni dhuluma kwa vijana kote ulimwengu… hii ndio maana tumempa Museveni makataa ya hadi Jumatatu kumwachilia huru Bobi Wine la sivyo tutaongoza maandamano makubwa nchini Kampala Jumatatu,” akasema Bw Owino ambaye ni Katibu Mkuu wa KYPC.

“Isitoshe, endapo kufikia Jumatatu dikteta Museveni hatakuwa amememwachilia mwenzetu tutavuruga shughuli katika ubalozi wa Uganda humu nchini. Tutaamuru kufungwa kwa ubalozi huo kwa sababu Kenya haiwezi kuendelea kushirikiana na taifa ambalo linakiuka haki za kibinadamu za rais wake,” akaongeza.

Naye Bw Okello alisema wao kama wanachama wa KYPC wamekuwa wakiwasiliana na wenzao nchini Uganda kupanga maandamano ya kulaani utawala wa Museveni.

“Wabunge vijana wenzetu nchini Uganda wanafahamu kuhusu mipango yetu na Jumatatu wako tayari kuungana nasi katika maandamano ya kutetea Bobi Wine. Kamwe hatuogopi kushikwa na polisi na wanajeshi,” akasema Mbunge huyo wa Nyando.

Bw Keter alisema ilisema ingekuwa bora kama Serikali ya Uganda ingemwasilisha Bobi Wine na kumfungulia mashtaka kwa mujibu wa sheria badala ya kumfungia korokoroni.

“Serikali ya Uganda kuendelea kumtesa mwenzetu, kumnyima chakula na hata huduma za wakili. Huu ni unyama ambao haufai kuendelea katika ulimwengu wa sasa,” akasema Mbunge huyo wa chama cha Jubilee.

Akaongeza: “Uganda ni mojawapo ya mataifa ya Jumuiya ya Afrika Mashariki na ambayo yametia sahihi mkataba wa kulinda haki za kibinadamu na kuheshimu utawala wa sheria. Kwa hivyo, hatutakubali haki kama hii kuendelea katika taifa hili jirani.”

Tangu wiki jana maafisa wa usalama wamekuwa wakipambana na mamia ya watu ambao wamekuwa wakiandamana nchini Uganda kupinga kukamatwa kwa Bobi Wine ambaye ni mbunge wa mrengo wa upinzani.

Watu kadhaa wameuawa na kujeruhiwa katika maandamano hayo huku wengine zaidi ya 100 wakikamatwa.

Bobi Wine alikamatwa wiki jana kwa madai kuwa alipatikana na bunduki kinyume cha sheria. Hatua hiyo ilichukulia muda mfupi baada ya msafara wa Rais Museveni kupigwa mawe na umati baada ya mkutano wa kampeni ya uchaguzi mdogo katika eneo la kaskazini mwa Uganda.

You can share this post!

Wabunge wapinga wakulima kupigwa msasa kabla ya kulipwa

Ruto na Waiguru wachemka kutajwa kuwa wafisadi zaidi

adminleo