Habari Mseto

Mbunge matatani kupokea Sh39 milioni za CDF

August 24th, 2018 1 min read

Mbunge wa Embakasi Kaskazini James Mwangi Gakuya (kulia laini ya umma) akiwa kortini Alhamisi. Picha/ EVANS HABIL

NA RICHARD MUNGUTI 

MBUNGE wa Embakasi kaskazini Bw James Mwangi Gakuya alishtakiwa pamoja na ndugu yake kwa kupokea zaidi ya Sh39milioni za hazina ya kustawisha eneo hilo la uwakilishi bungeni (CDF) kupitia miradi ya ujenzi wa barabara.

Bw Gakuya aliyetiwa nguvuni akiwa katika hafla ya kumbukumbu ya kifo cha hayati Mzee Jomo Kenyatta  alishtakiwa pamoja na  washukiwa wengine 11 mbele ya hakimu mwandamizi Bw Felix Kombo.

Mahakama ilimwachilia Mbunge huyo kwa dhamana ya Sh2milioni ama akishindwa kuilipa awasilishe mdhamini wa Sh5milioni.

Bw Gakuya , ndugu yake Patrick Waruingi Gakuya, Leah Waithera Guchu, Cleophas Omariba Oyaro, Richard Mwangi Chuchu,  Florence Ambura Njeri, Agnes Njeri Muthoni,Julius Maina Njoka,  Teresia Muthoni Macharia mmiliki wa kampuni ya Hunyu Bush Clearing and Bush Nuurseries, Stacey  ,Salome Nduta, kampuni za Mabaks Enterprises yao Mabw Gakuya na Tresmu Investments.

Washtakiwa walikanusha  mashtaka 27 dhidi yao kisha wakili Dunstan Omari akaomba waachiliwe kwa dhamana akisema “ hawatavuruga kesi kwa njia yoyote ile.”

Lakini ombi hilo lilipingwa vikali na viongozi wa mashtaka waliosema kuwa , “ washtakiwa wako na ushawishi mkubwa na watawatisha mashahidi walioorodheshwa kutoa ushahidi dhidi yao.”

Mbunge huyo alikabiliwa na mashtaka kwamba alitumia mamlaka yake na kampuni aliyokuwa anamiliki pamoja na nduguye kujipatia zaidi ya Sh39milioni kupitia ujenzi wa barabara kadhaa katika eneo hilo analowakilisha bungeni.

Mbunge huyo ,nduguye Waruingi  pamoja na kampuni yao Mabaks Limited walikbiliwa na shtaka la  kupokea kwa njia ya undanganyifu Sh19,691,772 kutoka kwa akaunti ya CDF ya Embakasi kaskazini.

Bw Oyaro alikabiliwa na mashtaka ya kukataa kuthibiti pesa za umma kwa kuruhusu pesa za umma zilipwe makampuni ambayo mbunge huyo alikuwa anahusika na umiliki wake.

Na wakati huo huo Bw Kombo aliwataka Waruinge na Stacey Wambui Njoki wafike kortini kujibu mashtaka kwa vile hawakuweza kufika.

Bw Kombo alielezwa washtakiwa hao hawakujua kuwa wanatakiwa kufika kortini kujibu mashtaka.