Wito Kenya iweke mikakati kukuza mastaa chipukizi
Kocha wa Rising Stars Gilbert Selebwa ameitaka Kenya kuwa mikakati ya muda mrefu ya kukuza chipukizi, utakaowezesha taifa kuwa na wachezaji wanaopanda kutoka timu za wadogo hadi wakubwa.
Selebwa alitoa ombi hilo baada ya matumaini ya Kenya kufuzu kwa fainali za mwakani za Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) kwa wachezaji wasiozidi miaka za 20, kufifia kufuatia sare ya 1-1 dhidi ya Sudan Kusini katika mechi yao ya mwisho ya kufuzu Kundi ‘C’ Jumamosi jijini Dar es Salaam.
“Watu wanapaswa kuelewa kwamba kujenga timu ina utaratibu wake. Hii ilikuwa mara yangu ya kwanza kunoa timu ya taifa na asilimia 70 ya wachezaji walikuwa wakicheza katika kiwango hiki kwa mara ya kwanza. Matarajio yalikuwa makubwa kutoka kwetu,” alisema Selebwa.
Alisema pia muundo wa kikosi hicho ulidhihirisha pengo lililopo katika mfumo wa Kenya wa kukuza vipaji vya vijana.
“Ukiangalia jinsi tulivyounda kikosi, asilimia 90 ya wachezaji hawakuwa wamecheza katika AFCON ya mwaka jana, huku wengi wao wakiwa wamepandishwa hadi timu za U20 na U23,” alisema.
Selebwa anaamini Kenya inahitaji kuwa na kundi thabiti la wachezaji wanaopitia hatua timu za chipukizi za timu za taifa za vijana badala ya kuunda vikosi wakati mashindano yanapokaribia.
“Tunapaswa kuwa na kundi maalum la wachezaji wanaopanda kutoka U15 hadi U17 na kisha U20 kwa sababu hilo ndilo tunalokosa,” alisema kocha huyo wa zamani wa AFC Leopards, Shabana FC na Muhoroni Youth.
Pia aliitaka Shirikisho la Soka Kenya (FKF) kuhakikisha makocha waliohitimu na wenye uwezo wanawekwa katika ngazi za chini ili kutambua na kukuza vipaji.
“FKF inahitaji kuwa na makocha sahihi wanaoshuka chini kuwanoa wachezaji. Hii itasaidia kuimarisha timu zetu za vijana,” aliongeza Selebwa.
Kenya ilimaliza kampeni yake ya kufuzu kwa AFCON bila ushindi baada ya kupoteza 2-0 dhidi ya Burundi katika mechi yake ya kwanza kabla ya kutoka sare ya 1-1 na Sudan Kusini.
Brighton Nancheri aliokoa pointi moja kwa Rising Stars kwa kusawazisha dakika ya 93 baada ya Sudan Kusini kupata bao kupitia Jonathan Ajoung dakika ya 26.
Matokeo hayo yaliiacha Kenya katika nafasi ya pili Kundi C ikiwa na pointi moja, sawa na Sudan Kusini lakini ikiwa mbele kwa tofauti ya mabao. Burundi iliongoza kundi hilo kwa pointi sita na kufuzu kwa nusu-fainali.
Kufuatia kutolewa huko, Kenya itakosa AFCON za mwaka ujao nchini Ghana.