Dimba

Mjiandae kwa sababu Chelsea tunakuja kivingine msimu huu, asema Kocha Alonso

Na MASHIRIKA September 1st, 2026 Kusoma ni dakika: 3

CHELSEA walikamilisha kampeni za Ligi Kuu ya Uingereza (EPL) msimu uliopita katika nafasi ya 10 jedwalini baada ya kujizolea jumla ya alama 52.

Kusuasua kwa kikosi hicho kulisukuma wasimamizi wake kuajiri mkufunzi Xabi Alonso kurithi mikoba iliyoachwa na kocha Liam Rosenior ambaye alimrithi Enzo Maresca.

Ujio wa Alonso ambaye ni raia wa Uhispania kulileta mseto wa utulivu, msisimko na uthabiti katika kambi ya Chelsea ambao sasa wanapigiwa upatu na wachanganuzi wa kabumbu kuwa mwiba kwa washindani wao wakuu katika soka ya Uingereza muhula huu.

Kikosi hicho kilifungua kampeni zake za msimu huu kwa ushindi wa 3-2 dhidi ya Fulham katika EPL ugani Craven Cottage mnamo Agosti 24 kabla ya kukomoa Luton Town 2-0 katika pambano la Carabao Cup siku tatu baadaye uwanjani Stamford Bridge.

Katika mchuano wao wa pili ligini muhula huu, Chelsea waliendeleza makali yao kwa kupepeta Brighton 4-3 nyumbani wikendi iliyopita na kusalia ndani ya mduara wa tatu-bora.

Ni matokeo yanayoweka hai matumaini yao ya kunyanyua takriban mataji yote ambayo wanapigania msimu huu yakiwemo EPL, Carabao Cup na Kombe la FA.

“Kikosi hakinipi sababu yoyote ya kutulia. Hatuko imara kabisa na utepetevu unadhihirika katika kila idara. Hatuko tayari kwa kibarua kinachotusubiri,” akasema Maresca kuhusu Chelsea walioambulia sare ya 1-1 dhidi ya Crystal Palace katika EPL, siku chache baada ya Servette FC ya Uswisi kuwatandika 2-1 mkondo wa pili wa mchujo wa Conference League.

Tangu waajiri Alonso, Chelsea wamepoteza mechi mbili pekee kati ya tisa. Hiyo ilikuwa mnamo Agosti 1 na Agosti 5 walipokubali kichapo cha 2-1 na 1-0 kutoka kwa Tottenham Hotspur na Juventus mtawalia katika mechi za kupimana nguvu.

Ingawa hivyo, masogora hao wa Alonso wamesalia imara katika EPL, wakijivunia sasa alama sita jedwalini sawa na limbukeni Hull City na miamba Manchester City.

Baada ya Chelsea kucharaza Brighton 4-3 mnamo Jumapili, kiungo wa zamani wa Blues na Spurs, Gus Poyet, 58, alisema itakuwa “aibu kubwa” iwapo Chelsea watashindwa kutwaa taji la EPL au angalau kufukuzana na Arsenal pamoja na Man-City hadi dakika ya mwisho kileleni mwa jedwali la ligi msimu huu.

Poyet anahisi kuwa usajili uliofanywa na Chelsea muhula huu tayari umeanza “kuzaa matunda” na kocha Alonso amedhihirisha kiu ya kunyanyulia waajiri wake mataji ya haiba.

“Maazimio ya Chelsea ni bayana kabisa. Wachezaji wao wameanza kuelewana na wanasuka pasi za hakika na haraka zinazoletea mashabiki msisimko mkubwa. Ni kikosi kisichotaka masihara kabisa muhula huu. Vijana hao watatamba na watakuwa tishio kwa takriban kila mpinzani,” akasema nyota wa zamani wa Crystal Palace na Brighton, Glenn Murray.

“Sawa na Arsenal, Manchester United, Man-City na Liverpool, Chelsea pia wana mseto wa chipukizi na wanasoka wazoefu wenye tajriba pevu. Hiyo itawafanya kuwa kivutio zaidi miongoni mwa mashabiki wa EPL katika kipindi cha mihula kadhaa ijayo,” akaongezea Murray.

“Wamiliki wa Chelsea wamewajibika kwa kusajili wachezaji mahiri. Kazi sasa ni kwa Alonso – akamilishe muhula huu katika angalau nafasi ya pili kisha atwae taji la EPL mnamo 2027-28 bila presha yoyote,” akasisitiza.

Baada ya kuachilia wanasoka Andrey Santos (Man-United), Nicolas Jackson (Aston Villa), Marc Cucurella (Real Madrid), Liam Delap (Nottingham Forest), Trevoh Chalobah (Como) na Tyrique George (Everton) muhula huu, Chelsea wamejisuka upya kwa kujinasia huduma za wachezaji 11.

Hao ni pamoja na Emiliano Martinez (Villa), Jordan Henderson (Brentford), Morgan Rogers (Villa), Valentin Barco (Strasbourg), Pep Chavarria (Rayo Vallecano) na Danny Welbeck (Brighton). Wengine ni Maxence Lacroix, Marco Palestra, Geovany Quenda, Dastan Satpaev na Emmanuel Emegha.

Alonso alinogesha EPL kwa kipindi cha miaka mitano akivalia jezi za Liverpool; na akasaidia miamba hao kushinda taji la Klabu Bingwa Ulaya (UEFA) mnamo 2005.

Aliwahi pia kusakatia Real Sociedad (1999-2004), Real Madrid (2009-2014) na Bayern Munich (2014-17) huku akitia kibindoni jumla ya mataji 14 kutokana na soka aliyotandaza katika ngazi ya klabu.

Alistaafu soka ya kimataifa mnamo Agosti 2014 baada ya kuchezea timu ya taifa ya Uhispania mara 114 na kuisaidia kunyanyua Kombe la Dunia la 2010 na mataji mawili ya Euro mnamo 2008 na 2012.

Aliwahi kudhibiti mikoba ya Bayer Leverkusen kwa kipindi cha miaka mitatu, akiongoza klabu hiyo ya Ujerumani kutwaa taji la kwanza la Bundesliga mnamo 2024 bila kushindwa, pamoja na German Cup (DFB-Pokal).

“Tunahitaji kushindana na ni lazima tujitume, tujitolee na kutia bidii katika kila idara. Ingawa ni vigumu kushinda kila mechi, ni muhimu kujiandaa kadri ya uwezo wetu kupigana kwa jino na ukucha. Huu ni msimu wetu,” akasema Alonso.