Habari Mseto

Bei ya mitumba kupanda serikali ikipendekeza ushuru mpya kwa waagizaji nchini

Na BENSON MATHEKA May 5th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

SERIKALI imependekeza ushuru mpya wa asilimia tano kwa mapato yanayotokana na uagizaji wa nguo zilizotumika maarufu kama mitumba, hatua inayoweza kuongeza gharama ya mavazi kwa mamilioni ya Wakenya.

Pendekezo hilo limo katika Mswada wa Fedha wa 2026 kupitia marekebisho ya Sheria ya Ushuru wa Mapato, likilenga watu binafsi wanaoagiza nguo, viatu na bidhaa zinazohusiana nazo chini ya kifungu cha ushuru nambari 6309.

Ushuru huo utatozwa wakati bidhaa zinaingizwa nchini kabla ya kuruhusiwa sokoni, na utachukuliwa kama ushuru wa mwisho.

Hatua hii ni sehemu ya juhudi pana za serikali kupanua wigo wa kukusanya ushuru hasa katika sekta isiyo rasmi pamoja na biashara ya uagizaji bidhaa kutoka nje.

Hata hivyo, wachambuzi wa masuala ya uchumi wanaonya kuwa ushuru huo mpya huenda ukaathiri moja kwa moja bei ya mitumba, bidhaa ambayo imekuwa tegemeo kuu kwa wananchi wa kipato cha chini na cha kati.

Kwa miaka mingi, mitumba imekuwa mbadala nafuu wa mavazi mapya, ikiwasaidia wengi kumudu gharama ya maisha inayozidi kupanda.

Wafanyabiashara wadogo, hasa katika masoko ya mijini na maeneo ya mashinani, wanaweza pia kuathirika pakubwa.

Kupanda kwa gharama ya uagizaji huenda kukawalazimu kuongeza bei ili kufidia ushuru huo, hali itakayoweza kupunguza mauzo na mapato yao.

Aidha, kuna hofu kuwa ongezeko hilo la bei linaweza kupunguza upatikanaji wa mitumba, na hivyo kuwaumiza zaidi raia wa kawaida wanaotegemea bidhaa hizo kwa matumizi ya kila siku.

Kwa upande mwingine, serikali inaamini kuwa hatua hiyo itasaidia kuongeza mapato ya ndani na kuhakikisha sekta ambayo kwa muda mrefu imekuwa nje ya mfumo rasmi wa ushuru inachangia ipasavyo katika maendeleo ya taifa.

Swali ni iwapo hatua hiyo itapata uungwaji mkono bungeni na jinsi itakavyotekelezwa bila kuwaumiza zaidi wananchi wa kawaida.

Wengi sasa wanasubiri kwa hamu kuona hatima ya pendekezo hilo na athari zake kwa soko la mitumba nchini.