• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 4:42 PM
JUBILEE: Tuju athibitisha kikao cha Rais Kenyatta na maseneta Ikuluni Jumatatu

JUBILEE: Tuju athibitisha kikao cha Rais Kenyatta na maseneta Ikuluni Jumatatu

Na CHARLES WASONGA

KATIBU Mkuu wa Jubilee Raphael Tuju amethibitisha kuwa maseneta wa chama hicho wamealikwa na Rais Uhuru Kenyatta kwa mkutano katika Ikulu ya Nairobi, Jumatatu, Mei 11, 2020.

Hatua hiyo inajiri baada ya wabunge na maseneta wanaoegemea mrengo wa Naibu Rais Dkt William Ruto kuwa katika malumbano ya mara kwa mara na wenzao wanaoegemea mrengo wa Rais Kenyatta.

Kimsingi, uhusiano wa Rais Kenyatta na Dkt Ruto haujakuwa mzuri na wa karibu katika siku za hivi karibuni kwani wawili hao hawajakuwa wakionekana pamoja kwa kipindi kirefu.

Wandani wa Dkt Ruto wamekuwa wakimshinikiza Rais Kenyatta aitishe mkutano wa Kundi la Wabunge (PG) wa Jubilee ili kujadili masuala ambayo yamekuwa yakileta mgawanyiko ndani ya chama hicho tawala.

Bw Tuju amenukuliwa akisema kuwa suala kuu ambalo litajadiliwa ni kuhamishwa kwa baadhi ya majukumu ya Kaunti ya Nairobi hadi Serikali Kuu, ambalo limezua utata.

“Hii ndiyo sababu Rais amewaalika maseneta pekee wala sio wajumbe wa Bunge la Kitaifa, kwani maseneta ndio hushughulikia masuala ya ugatuzi,” amesema Bw Tuju.

Hata hivyo, Katibu huyu Mkuu amefafanua kuwa mwaliko wa mkutano huo ulitoka moja kwa moja kwa Rais Kenyatta na “hivyo siwezi kuelezea mengi kuhusu ajenda yake.”

Mkutano huo unatarajiwa kuanza saa mbili na nusu asubuhi.

“Mnavyojua ni kwamba ni Rais mwenyewe aliyewaalika maseneta. Kwa hivyo, siwezi kutoa mwelekeo kuhusu masuala yatakayojadiliwa. Lakini kila ninachofahamu ni kwamba hali katika Kaunti ya Nairobi itajadiliwa kutokana na shida ambazo zimeizonga tangu kuhamishwa kwa baadhi ya majukumu kwa serikali kuu,” Tuju ameeleza.

Nairobi

Ingawa amehiari kuachilia majukumu manne makuu ya kaunti hiyo yaendeshwa na Serikali Kuu kwa kutia saini muafaka wa kufanikisha hilo Februari 2020 Gavana Mike Sonko alibadili msimamo juzi.

Anadai Serikali Kuu ilivuka mipaka na kutaka kusimamia hata yale majukumu ambayo yalifaa kusalia chini ya usimamizi wa serikali yake.

Kwa hivyo, ametisha kusambaratisha shughuli katika Kaunti hiyo kwa kujiondoa kutoka muafaka huo.

Hii ndiyo maana Aprili, Sonko alidinda kutia saini mswada ambao ulipendekeza Sh15 bilioni zitengewe mamlaka ya Nairobi Metropolitan Services (NMS) iliyobuniwa na Rais Kenyatta kuendesha majukumu hayo kwa niaba ya Serikali Kuu.

Hatua hiyo ilichangia mgongano kati yake na Ikulu na kuchangia kuondolewa kwa walinzi wake na baadhi ya madereva waliokuwa wakimhudumia.

Maseneta wakiongozwa na Kiongozi wa Wengi Kipchumba Murkomen pia wamepinga hatua ya Serikali Kuu kuwapeleka wanajeshi kusimamia NMS.

Afisi hiyo inaongozwa na Meja Jenerali Mstaafu Mohammed Badi kama Mkurugenzi Mkuu. Na majuzi Serikali Kuu iliwatuma maafisa wanne zaidi katika makao makuu ya kaunti ya Nairobi, City Hall.

Mkutano wa mwisho wa PG wa Jubilee ulifanyika mnamo 2017 baada ya Rais Kenyatta kushinda uchaguzi na kuanza kipindi chake cha pili na cha mwisho. Ni katika mkutano huo ambapo wenyeviti na manaibu wenyeviti wa kamati za bunge la kitaifa na seneti waliteuliwa.

You can share this post!

COVID-19: Kenya yathibitisha visa 23 vipya idadi jumla...

Askofu akamatwa waumini wakitoroka Mikindani

adminleo