Habari

Onyo kali latolewa kwa machifu wazembe Pwani

Na KALUME KAZUNGU April 27th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MACHIFU Pwani wameonywa dhidi ya kutowajibika kazini huku wakitakiwa kuhakikisha watoto wote kwenye maeneo yao wanaenda shule.
Shule zote kote nchini zinafunguliwa Jumamatu kuanza muhula wa pili ambao ndio mrefu zaidi mwaka huu.
Akizungumza wakati alipokamilisha ziara yake ya wiki nzima Lamu, Mratibu wa Usalama Ukanda wa Pwani, Bi Rhoda Onyancha aliwakashifu baadhi ya machifu wa Lamu na kaunti zingine za Pwani kwa kuzuia utekelezaji wa sera ya elimu ya mpito wa asilimia 100.
Aliwaonya machifu, manaibu wao na hata makamishna na manaibu wao kwamba hatua kali zitachukuliwa dhidi yao endapo kutapatikana watoto wa umri wa kwenda shule wakirandaranda mitaani kwenye maeneo yao badala ya kuwa madarasani kusoma.
Bi Onyancha alishikilia kuwa sera ya elimu ya mpito wa asilimia 100 ni mpango wa serikali kuhakikisha kila mwanafunzi aliyemaliza shule ya msingi (KCPE) au Sekondari Msingi (JSS) wanahamia au kuendeleza ngazi zinazofuata za elimu.
Alishikilia kuwa serikali ya kitaifa na hata zile za kaunti zimejitahidi kimiundomsingi na kwamba hakuna sababu ya mtoto wa umri wa kwenda shule kusalia nyumbani.

Ili kutimiza malengo ya mpito wa asilimia 100 ya wanafunzi wanaojiunga na shule au kupanda ngazi zao, Bi Onyancha alisema serikali kuu imehakikisha elimu ni bure shuleni.

“Hivyo sitamvumilia chifu au kamishna yeyote atakayezembea kimajukumu, hasa endapo wanafunzi wataonekana wakizurura ovyo kwenye mitaa yenu shule zinapofunguliwa. Serikaliza kaunti,ikiwemo gavana Issa Timamy hapa, zimetujengea madarasa ya chekechea (ECDE). Tuhakikishe yanajaa wanafunzi,” akasema Bi Onyancha.
Mara nyingi kumeshuhudiwa watoto wadogo wa umri wa kwenda shule wakishiriki shughuli za uvuvi baharini Pwani, hasa kaunti ya Lamu, hali ambayo Bi Onyancha alisisitiza kwamba lazima ikome.
Alieleza kutoridhishwa kwake na kuwepo kwa magenge ya mapanga Pwani ambapo wengi wa wahalifu wanaounda au kuhusika na magenge hayo ni vijana wadogo.
“Hata wengine wanafaa kuwa shuleni. Lazima tukumbatie elimu ili kuzuia uozo kama huo kutokea kwenye jamii zetu. Machifu lazima tuwajibike la sivyo mzivue hizo sare na kofia zenu tuwape watu watakaowajibikia majukumu kazini,” akasema Bi Onyancha.
Naye Kamishna wa Kaunti ya Lamu, Bw Wesley Koech alimhakikishia mshirikishi huyo wa usalama Pwani kwamba mipango kabambe ipo kuhakikisha hakuna mtoto atakayesalia nyumbani muhula wa pili unapoanza.
Bw Koech alitangaza mpango wa kuzindua msako wa nyumba kwa nyumba na kuhakikisha wanafunzi wote wanaenda shule kuanzia Jumatatu.
“Mimi binafsi nitakuwa hapa kisiwani Lamu. Nitashirikiana na hawa machifu wetu kuingia nyumba moja hadi nyingine ilmuradi tuhakikishe hakuna mwanafunzi anabaki nyuma shule zinapofunguliwa Jumatatu,” akasema Bw Koech.
Aliongeza, “Tukimpata mtoto nyumbani Jumatatu, tutamchukua na kumpeleka shule. Kisha tukirudi mara ya pili na tupate mtoto wako anazurura mtaani ama kusalia nyumbani, tutakukamata wewe mzazi na kukuchukulia hatua kwa kutowajibikia jukumu lako.”