Anguka Nayo! Wanamuziki hawataongezwa pesa nyimbo zao zikichezwa kwenye mikutano ya kisiasa
WABUNGE wamekataa pendekezo la wanamuziki la kutaka waongezewa malipo wanayopata kila mara nyimbo zao zinapochezwa katika mikutano ya kisiasa.
Wiki hii, wabunge walipitisha ripoti ya Kamati ya Bunge kuhusu Sheria Ndogo iliyopendekeza kufutiliwa mbali kwa viwango vipya vya ushuru wa muziki kwa madai kuwa vinakiuka Katiba kwa kuzuia haki ya wananchi kushiriki shughuli za kisiasa.
Kamati hiyo ilisema ada zilizotozwa kwa shughuli za kisiasa kama uzinduzi wa vyama, wagombea na manifesto zingewaongezea wananchi mzigo mkubwa wa kifedha na hivyo kuathiri haki zao za kisiasa chini ya Kifungu cha 38 cha Katiba.
Viwango hivyo vipya vilichapishwa Januari 29, 2026 baada ya kuidhinishwa na Waziri wa Masuala ya Vijana, Uchumi wa Ubunifu na Michezo Salim Mvurya.
Pendekezo hilo lingewanufaisha wanamuziki huku taifa likielekea kipindi cha kampeni kali kabla ya uchaguzi mkuu wa 2027.
Chini ya ushuru huo mpya uliokataliwa, wagombea urais wangetozwa Sh500,000 kutoka Sh400,000 za sasa, wagombea ugavana Sh200,000 huku wale wa useneta wakilipa Sh150,000 kutoka Sh100,000.
Ada za wagombea ubunge, wawakilishi wa wanawake na MCA zingepandishwa hadi Sh100,000.
Vyama vya kisiasa vingelipa ada ya kila mwaka ya Sh600,000 kutumia muziki katika mikutano ya kampeni na shughuli nyingine za kisiasa.
Kamati hiyo ilisema ushuru huo haukuwa wa haki kwa sababu uliweka viwango vya jumla bila kuonyesha uhusiano wa moja kwa moja kati ya ada hizo na matumizi ya hakimiliki.
Wabunge pia walikosoa mchakato wa ushirikishaji wa umma wakisema haukuwa wa kutosha wala wenye uwazi kama inavyotakiwa na Katiba.
Bodi ya Haki Miliki Kenya (KECOBO) ilisimamia utayarishaji wa ushuru huo kwa kushirikiana na mashirika ya usimamizi wa hakimiliki.
Hata hivyo, Mahakama Kuu mwaka jana ilibatilisha viwango vya awali vya 2023 kutokana na ukosefu wa ushirikishaji wa umma wa maana na kuagiza KECOBO kufanya mashauriano mapya kabla ya kuwasilisha ushuru wowote mpya bungeni.