Jamvi La Siasa

Huenda Ruto akawafuta kazi mawaziri ‘wataalamu’ wa ODM

Na CECIL ODONGO May 24th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

LICHA ya wito kutanda kuwa mawaziri John Mbadi (Fedha) na Opiyo Wandayi (Kawi) wajiuzulu wakati wa maandamano ya kupinga bei ya juu ya mafuta wiki hii, maswali yameibuka iwapo Rais William Ruto ana uhuru wa kuwatimua mawaziri wa ODM au lazima kwanza ashauriane na uongozi wa chama hicho .
Kando na wawili hao, mawaziri wengine ‘wataalamu’ ambao ODM iliipa Serikali Jumuishi ni Hassan Joho (Madini), Beatrice Askul (Jumuiya ya Afrika Mashariki) na Wycliffe Oparanya (Vyama vya Ushirika).
Mawaziri hao waliteuliwa Julai 2024 wakati wa kilele cha maandamano ya kizazi cha Gen-Z na wakaapishwa Agosti mwaka huo.
Uteuzi wao ulifuatia muafaka kati ya Rais William Ruto na marehemu Kiongozi wa ODM Raila Odinga ambao ulisambaratisha maandamano dhidi ya Mswada wa Fedha 2024.
Wakati wa maandamano ya juzi mawaziri Mbadi na Wandayi walikashifiwa kwa kukosa kuonyesha ‘utaalamu’ wao katika kusaka muafaka na wahudumu wa matatu.
Mbadi hata alihoji kwamba walikuwa wakisubiri Rais Ruto atoke ziara yake nchini Kazakhstan ili kushauriana na wahudumu hao.
Wandayi naye akiwa Wajir alionekana kulemewa na suala hilo la bei ya mafuta akiomba subira na amani.
Kutokana na kulemewa kwa Wandayi kinara wa Wiper Kalonzo Musyoka Jumatatu alimtaka ajiuzulu.
“Anastahili achukue hatua ambayo Wakenya watamkumbuka nayo kutokana na kushindwa kushusha bei ya mafuta na kuzima mgomo wa wahudumu wa matatu. Bw Wandayi anafaa kuwa na ujasiri na kujiuzulu wadhifa wake,” akasema Bw Musyoka kwenye taarifa kwa vyombo vya habari.
Je Mabw Mbadi na Wandayi wanaweza kutimuliwa na Rais Ruto ndani ya Serikali Jumuishi?
Kifungu 152 cha Katiba kinampa Rais mamlaka ya kuwafuta mawaziri. Kifungu cha 152 (5) kinasema afisi ya waziri itasalia bila mshikilizi iwapo atafutwa kazi na rais.
Katika makubaliano kati ya Rais Ruto na marehemu Bw Odinga, hakuna kifungu chochote kinachomzuia Rais Ruto kuwafuta kazi mawaziri wanaohudumu serikalini mwake.
Je, anapaswa kushauriana na kiongozi wa ODM, Seneta Oburu Oginga, iwapo ataamua kuwaondoa baadhi ya mawaziri wa chama hicho kutoka nyadhifa zao?
Kulingana na Seneta wa Kakamega Boni Khalwale, Mabw Mbadi, Wandayi walipaswa kuondoka serikalini kitambo, hasa baada ya mafuta chafu kuingia sokoni.
“Katiba iko wazi kuhusu mamlaka ya uteuzi, na kwa vyovyote vile hakuna utaalamu wowote ambao Mabw Mbadi na Wandayi wameleta katika baraza la mawaziri,” Bw Khalwale akaambia mwandishi huyu.
“Suala hili la kuleta uthabiti serikalini halina msingi wowote. Kwa kweli, kundi la Linda Mwananchi ndilo pekee linaweza kufanya hivyo, si Oburu. Nahimiza Bunge la Kitaifa kuanza mchakato wa kuwaondoa Mabw Mbadi na Wandayi, na pia nawashauri wawili hao waondoke kabla ya kufutwa au kuhamishwa,” akaongeza.
Wakili wa marehemu Raila, Paul Mwangi, naye anasema kuwa “wataalamu” hao hawakujiunga na serikali kama wawakilishi wa ODM. Anasema Rais ana mamlaka ya kuwafuta kazi au kuwahamisha kwa hiari yake.
“Waliachiliwa kwenda kufanya kazi, na ilitarajiwa kwamba baada ya kujiunga na serikali mazungumzo zaidi kuhusu ushirikiano yangefanyika, lakini hilo halikutokea,” akasema wakili huyo katika mahojiano ya simu.
“Kisiasa, itakuwa busara kwa Ruto kushauriana na ODM, lakini hakuna kitu kinachomzuia kisheria kuchukua hatua yoyote anayoona inafaa,” akaongeza Bw Mwangi, huku akikiri kuwa ni Raila aliyewasilisha majina ya mawaziri hao watano kujiunga na serikali.
Aliendelea kusema kuwa kulikuwa na matarajio kwamba vyama vingine vya kisiasa pia vingejiunga na serikali, lakini viongozi wao walibadilisha msimamo.
Kwa mujibu wa Kiongozi wa Vijana wa ODM, John Ketorah, mawaziri wa ODM hawawezi kufutwa kazi au kuhamishwa bila mashauriano na idhini ya Dkt Oginga.
“Tulipata nafasi hizi kwa sababu tulileta uthabiti serikalini, na hata kama watahamishwa, lazima ODM ipewe nafasi zenye hadhi kama wizara tulizonazo sasa,” akasema Bw Ketorah.
“Njia pekee ya kutoka kwenye nafasi hizi ni ikiwa baraza lote la mawaziri litavunjwa kama ilivyotokea wakati wa maandamano ya Gen Z. Chochote kitakachowapata Mbadi, Wandayi na mawaziri wengine lazima kifanyike kwa idhini ya Dkt Oburu,” akaongeza.
Mchanganuzi wa siasa Salim Odeny anadai kuwa Mabw Mbadi Wandayi na mawaziri wengine wa ODM waliingia serikalini kwa haraka bila idhini ya Raila.
Bw Odeny anaongeza kuwa baadaye Raila aliwapa barake zake kuzua mgawanyiko na kudumisha umoja wa chama.
“Kwa hali ilivyo sasa, Oburu lazima ashauriwe kwa sababu ODM ilijihusisha nao walipoingia serikalini. Hata hivyo, Mbadi atakuwa na changamoto kubwa zaidi kutokana na azma yake ya kuwa kinara wa siasa za Waluo na ushindani alionao na familia ya Raila,” akasem Bw Odeny.
“Siwezi kusema wamekuwa na utendakazi duni kwa sababu wamejikuta katika serikali yenye changamoto nyingi za kiuchumi. Wanaweza kuhamishwa, na iwapo wataondolewa kabisa, wale watakaowachukua nafasi lazima watoke ODM,” akaongeza
 Katika ziara zake mbalimbali za kisiasa Nyanza, Rais Ruto amekuwa akimsifu mara kwa mara Bw Mbadi, akimtaja kuwa mchapa kazi na mwenye mchango mkubwa katika kuboresha uchumi wa nchi.
“Nataka kuwashukuru kwa kunipa waziri Mbadi ambaye ni mwerevu na mchapa kazi. Nafanya kazi na Mbadi kwa urahisi mkubwa kwa sababu anaelewa mambo haraka, anaijua siasa, na anajua jinsi ya kushughulikia masuala mbalimbali,” alisema Rais Ruto alipokuwa akihutubia wananchi kwenye mkutano wa maombi katika Shule ya Upili ya Agoro Sare, eneo la Kasipul, Machi 22, 2026.