Bajeti: Simu za mkononi kuendelea kuwa ghali nchini
WIZARA ya Fedha imebadili msimamo wake kuhusu mpango wa kuondoa ushuru wa forodha wa asilimia 25 unaotozwa simu za mkononi zinazoagizwa kutoka nje, hatua inayomaanisha kuwa Wakenya wataendelea kununua simu kwa bei ya juu.
Awali, serikali ilikuwa imepanga kufuta ushuru huo pamoja na ushuru wa ongezeko la thamani (VAT) wa asilimia 16, ada za kuagiza bidhaa ya asilimia 2.5 na ushuru wa maendeleo ya reli wa asilimia mbili.
Hatua hiyo ingeacha simu zikitozwa ushuru wa asilimia 25 pekee baada ya ushuru huo kuongezwa kutoka asilimia 10 hadi 25.
Hata hivyo, Waziri wa Fedha, John Mbadi, aliposoma bajeti bungeni Alhamisi, alithibitisha tu kuondolewa kwa baadhi ya ushuru huo lakini hakutaja mpango wa kufuta ushuru wa forodha wa asilimia 25.
Badala yake, Mbadi alisema Kenya imewasilisha ombi kwa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) ili iruhusiwe kuondoa ushuru wa forodha kwa malighafi na vipuri vinavyotumika kuunganisha simu za kisasa nchini.
Hatua hiyo inalenga kulinda sekta ya uundaji wa simu nchini lakini ina maana kuwa simu zinazoagizwa kutoka nje zitaendelea kuwa ghali.
“Ili kuimarisha uunganishaji wa kidijitali kama sehemu ya nguzo ya mpango mkuu wa kidijitali katika Ajenda ya Mabadiliko ya Kiuchumi kutoka Chini kwenda Juu (BETA), uunganishaji wa vifaa vya kisasa nchini unasalia kuwa kipaumbele kikuu,” Mbadi aliambia Bunge la Kitaifa.
Aliongeza kuwa kuongeza upatikanaji wa vifaa vya mawasiliano vya bei nafuu kutawawezesha Wakenya wengi kushiriki katika uchumi wa kidijitali na kunufaika na fursa mpya za biashara na ubunifu.
Awali wizara ilikuwa imetetea uamuzi wa kuongeza ushuru wa bidhaa kwa simu hadi asilimia 25 huku ikiahidi kupunguza ushuru mwingine ili kurahisisha mfumo wa ulipaji kodi.
Lakini kwa kuwa Kenya ni mwanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, haiwezi kuondoa ushuru wa forodha peke yake.
Badala yake, ni lazima iombe Baraza la Mawaziri la EAC kuidhinisha msamaha huo kulingana na malengo ya kiuchumi na kifedha ya nchi.
Kwa mujibu wa Waziri Mbadi, mapendekezo ya ushuru yaliwasilishwa bungeni Mei 8 na baadaye kupelekwa EAC Mei 15, lakini ombi la kuondoa ushuru kwa simu zinazoagizwa kutoka nje halikuwemo.