Makala ya mwaka huu ya Safaricom Chapa Dimba yazinduliwa
MAKALA ya tano ya michuano ya Safaricom Chapa Dimba, yalizinduliwa rasmi Jumamosi katika Uwanja wa Kimataifa wa Jomo Kenyatta, Kisumu.
Katika msimu huu mpya, wachezaji bora 32 watakaochaguliwa kutoka mashindanoni ya mwaka huu watapata nafasi ya kuiwakilisha Kenya kwenye dimba la Kombe la Gothia nchini Uswidi.
Mbali na michezo, Safaricom imeweka mkazo mkubwa kwenye elimu ambapo vijana 150 bora watanufaika na ufadhili wa masomo ya juu kupitia mpango wa Citizens of the Future.
Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Mkurugenzi Mkuu wa Safaricom PLC Peter Ndegwa alisema kampuni hiyo inalenga kutumia michezo, elimu na teknolojia kubadilisha maisha ya vijana nchini.
“Tunataka kukuza si tu wanasoka bora, bali vijana waliokomaa na wenye uwezo wa kuleta mabadiliko nchini,” alisema Ndegwa ambaye aliandamana na viongozi wa Shirikisho la Soka nchini (FKF) akiwemo ras wa shirikisho hilo Hussein Mohammed.
Katika mabadiliko mapya, waandalizi wamepunguza umri wa washiriki kutoka miaka 16-20 hadi 15-18 ili kuwezesha vipaji kugunduliwa mapema na kupata nafasi katika soka ya kulipwa nchini na kimataifa.
Safaricom pia imeongeza matumizi ya teknolojia katika usajili na uchambuzi wa wachezaji. Baada ya mafanikio ya matumizi ya vifaa vya AI na GPS msimu uliopita, safari hii kampuni hiyo italeta kamera za VeO pamoja na vifaa vya MyScout AI kuanzia ngazi ya kaunti.
Teknolojia hiyo itasaidia kufuatilia wachezaji, kasi, nafasi wanazocheza na kiwango chao cha mchezo huku ikiwajengea wasifu wa kidijitali utakaoweza kuonekana na maskauti wa kimataifa.
Mashindano hayo yatafanyika katika maeneo manane nchini katika ngazi ya wadi, kaunti, mikoa na fainali ya kitaifa.
Usajili wa timu za wavulana na wasichana umefunguliwa kupitia tovuti ya Safaricom Chapa Dimba
Washindi wa kitaifa katika kila kundi watajinyakulia Sh1 milioni huku zawadi nyingine zikitolewa katika ngazi za kaunti na mikoa pamoja na tuzo za mfungaji bora, kipa bora na mchezaji bora.
Tangu kuanzishwa mwaka 2017, mashindano hayo yamelea mastaa kadhaa wanaocheza soka ya kulipwa akiwemo Benson Omalla, Bryton Otieno, Austine Odongo, Derrick Oketch, Jentrix Shikangwa, Marion Serenge na Mercy Akoth.
Baadhi ya nyota hao pia wameiwakilisha Kenya katika mashindano ya kimataifa yakiwemo Kombe la Dunia la Mabinti la wachezaji chini ya miaka 17.
Mashindano hayo yanaandaliwa kwa ushirikiano na FKF kama sehemu ya juhudi za kukuza soka ya vijana mashinani nchini Kenya.