Gaucho atetea uteuzi wake, asema ingawa ana kisomo haba, anayo hekima
MWANAHARAKATI Calvince Okoth maarufu kama ‘Gaucho’ ametetea uteuzi wake kwenye Bodi ya Hospitali ya Mama Lucy akisema atawaonyesha wanaokosoa uteuzi wake kuwa ni mchapakazi.
Hatua ya Gavana Johnson Sakaja kumteua Bw Okoth pamoja na wanamuziki wa Benga Kennedy Wambua Ngunze maarufu kama Ken wa Maria na Triza Miroya kuliibua malalamishi mitandaoni.
Bw Gaucho ni mwanaharakati na mfuasi sugu wa ODM huku Bw Wa Maria na Bi Miroya wakiwa wanachama kindakindaki wa UDA.
“Namshukuru Mungu na pia marehemu Raila Odinga ambaye aliashiria uteuzi huu miaka mitatu iliyopita. Pia namshukuru Bw Sakaja na naamini uteuzi huu utawapa vijana motisha kuwa bado wanaweza kufanikiwa licha ya eneo wanalotoka,” akasema kwenye mahojiano.
Alifichua kuwa marehemu Raila Odinga alikuwa amemshauri awajibikie jukumu la kumpa mshahara kila mwezi huku akihudumia jamii kwenye kiwango cha kaunti au kitaifa.
Bw Gaucho hapo awali alikuwa akilipwa mshahara na Wakfu wa Jaramogi Oginga Odinga hadi mauti ya Raila ambapo mambo yalibadilika.
Alifichua kuwa alikuwa akidhani uteuzi huo ulikuwa mzaha hadi pale alipopigiwa simu na Mama Ida Odinga, mkewe Raila kumpongeza.
“Aliniambia alifurahia hatua nilizokuwa nimepiga na akaniambia nisaidie jamii, nisimamie haki na nisiruhusu watu wadhulumiwe,” akasema.
Uteuzi wake ulishutumiwa kutokana na kisomo chake haba lakini Bw Gaucho anasema kuhudumu kwenye bodi kunahitaji hekima na maelewano badala ya elimu ya shule.
“Wale ambao wana shaka nami wanipe muda kwa sababu nitawatetea watu na kupigania haki zao. Sitanyamaza,” akasema.