Hofu yatanda Mashariki ya Kati Amerika na Iran zikitoleana vitisho tena
WASHINGTON/CAIRO
HOFU ilitanda Jumatatu kwamba huenda makubaliano ya kuzimwa kwa uhasama kati ya Amerika na Iran yakakosa kufikiwa baada ya Amerika kusema ilinasa na kulemaza meli moja ya Iran kwa kuvuka kuzuizi chake.
Iran nayo imeapa kulipiza kisasi kutokana na kitendo hicho cha Amerika.
Isitoshe, juhudi za kupatikana kwa amani ya kudumu Mashariki ya Kati zilionekana kuyumbayumba baada ya Iran kusema haitashiriki katika awamu ya pili ya mazungumzo na Amerika iliyotarajiwa kuanza jana jioni kabla ya kipindi cha usitishwaji vita kukamilika leo, Aprili 21, 2026.
Amerika imeendelea kuweka vizuizi katika bandari za Iran, ilhali Iran ilifungua na kisha kufunga tena Mkondo wa Hormuz, unaotumika kupitishia karibu asilimia 20 ya mafuta yanayosambazwa ulimwenguni.
Jeshi la Amerika lilisema mnamo Jumapili, Aprili 19, kwamba ilishambulia meli moja ya mizigo ya Iran, ilipokuwa ikielekea bandari ya Bandar Abbas, na kulemaza injini zake.
“Tumedhibiti meli yao na tunaona mizigo iliyobeba,” Rais wa Amerika Donal Trump aliandika katika mitandao ya kijamii.
Jeshi la Iran lilisema meli hiyo ilikuwa ikisafiri kuelekea China.
“Tunaonya kwamba wanajeshi wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran hivi karibuni watajibu na kulipiza kisasi dhidi ya kitendo cha uharamia cha jeshi la Amerika,” msemaji mmoja wa jeshi akasema, kulingana na shirika la habari la kitaifa Iran.
Bei ya mafuta ilipanda kwa zaidi ya asilimia 5 na masoko ya hisa yakashuhudia misukosuko huku wafanyabiashara wakiingiwa na wasiwasi kwamba makubaliano ya kusitishwa kwa vita yataporomoka na uchukuzi kuingia na kuondoka Ghuba utaendelea kukwama.
Shirika la Habari la Iran limeripoti kwamba nchi hiyo imekataa kushiriki katika awamu ya pili ya mazungumzo ya amani jijini Islamabad, Pakistan ikitaja hatua ya Amerika kuendelea kuweka vizuizi katika bandari zake, kutoa kauli za vitisho na mwenendo wa Amerika kubadilisha misimamo yake kila mara huku ikiweka “masharti magumu”.
“Mtu hawezi kuzuia Iran kuuza mafuta nje huku akitarajia tutoe nafasi kwa nchi zingine kusafirisha mafuta na bidhaa nyinginezo,” Makamu wa Rais wa Kwanza wa Iran Mohammadreza Aref akaandika katika mitandao ya kijamii.
“Chaguo ni hili; aidha soko huru ya mafuta kwa wote au hatari ya gharama kubwa kwa wote.” akaongeza.
Awali, Trump alikuwa ameonya Iran kwamba Amerika ingeharibu kila daraja na kila kiwanda cha kuzalisha kawi nchini humo ikiwa Iran itakataa masharti yake, akionekana kuendeleza mtindo wa kutoa vitisho.
Nayo Iran imesema ikiwa Amerika itashambulia miundo msingi yake, itashambulia vituo vya kuzalisha kawi na viwanda vya kutakasa maji katika mataifa jirani eneo hilo la Ghuba.
Mnamo Jumapili, Rais Trump alisema wajumbe wake wangewasili jijini Islamabad jana jioni, siku moja kabla ya kipindi cha majuma mawili cha usitishwaji vita kukamilika.
Afisa mmoja wa Ikulu ya White House alisema ujumbe wa Amerika utaongozwa na Makamu wa Rais J.D Vance.
Vance ndiye aliongoza ujumbe Amerika ulioshiriki katika awamu ya kwanza ya mazungumzo hayo ya amani wiki moja iliyopita.
Katika ujumbe huo pia alikuwepo balozi wa Trump Steve Witkoff na mkaza mwana wake Jared Kushner.