Hali si hali Mombasa mafuriko kwingi kufuatia mvua ya siku tatu
USAFIRI katika maeneo kadha ya Kaunti ya Mombasa umevurugika kufuatia mvua kubwa iliyonyesha kwa siku tatu zilizopita.
Hali hiyo ilisababisha barabara kufurika, baadhi ya nyumba kuingia maji, na biashara nyingi kushindwa kufunguliwa.
Katika ukaguzi uliofanywa na Taifa Leo mnamo Alhamisi, baadhi ya barabara mjini humo zilikuwa zimejaa maji hali iliyosababisha msongamano mkubwa.
Baadhi ya wakazi waliokuwa wanaelekea kazini na shuleni walilalamikia kuchukua saa nyingi kufika walikoenda.
“Nimetoka nyumbani saa moja asubuhi, saa moja baadaye bado sijafika kazini,” alisema Bi Alice Mwema, mkazi wa VOK.
Maeneo yaliyoathirika na mvua ni Nyali, Kisauni, Bamburi na sehemu za Changamwe.
Madereva na abiria walilazimika kupita katika maji yaliyowafikia magotini huku magari ya uchukuzi wa umma (matatu) yakipandisha nauli, kutokana na msongamano uliowasababishia kuchelewa.

Picha|Kevin Odit
Watoto wadogo waliokuwa wakielekea shuleni walibebwa mgongoni na mama zao ili kuwavusha katika maji hayo. Wale waliokuwa wakubwa walitembea huku wakiwa wamebeba viatu vya shule mikononi wakijitahidi kuwahi masomo yao.
Katika barabara kuu ya Mombasa-Malindi ambayo hupitisha magari mengi, mkondo mmoja tu ndio uliweza kupitika baada ya maji ya mvua kufunika mashimo na sehemu za pembeni mwa barabara.
Madereva walilazimika kusonga taratibu katika maeneo yaliyojaa maji, huku baadhi ya magari yakikwama na mengine yakiteleza kwenye lami iliyofunikwa na matope.
“Ni hatari kuendesha gari barabara hii kwa sasa. Mashimo hayaonekani kabisa. Unaweza kudondoka moja kwa moja ndani na kusababisha ajali mbaya,” alisema Bw Ali Suleiman, dereva wa matatu anayehudumu kati ya Bombolulu na Ferry.
Bw Suleiman alisema wamepandisha nauli kutokana na foleni ndefu na matumizi makubwa ya mafuta.
“Kawaida tunatoza Sh70 kutoka Bombolulu hadi Ferry, lakini sasa tunalazimika kutoza Sh100 ili kufidia hasara ya mafuta na muda tunaopoteza njiani. Hii si tamaa, ni hali ya kujikimu,” aliambia Taifa Leo.
Bi Mary Achieng’, mkazi wa Mtopanga, alilalamikia kupanda kwa nauli akisema hali ya maisha ni ngumu mno.
“Nilikuwa nalipa Sh100 kutoka Mtambo hadi Ferry, sasa ni Sh150. Na bado hujui kama utawahi kufika salama, kwani magari huharibika au hukwama njiani. Uchumi ni mgumu,” alisema.
Si abiria pekee wanaoumia. Wakazi wengi wanasema wamechoshwa na miaka mingi ya mipango mibovu na ukosefu wa hatua za dharura kutoka kwa serikali.
Wanatoa wito kwa serikali ya kaunti kuwachukulia hatua wamiliki wa nyumba waliovamia njia za maji na kujenga kwenye maeneo ya kupitia maji.
“Majengo mengi yamejengwa juu ya njia asilia za maji kwenda baharini, jambo ambalo huzuia maji kutiririka kwa uhuru. Kila mvua ikinyesha, hali huwa mbaya zaidi,” alisema Bi Easther Wamboi, mama wa watoto watatu kutoka Kisauni.
Aidha, Bi Wamboi alihimiza serikali kuimarisha mifumo ya mabomba ya kupitishia maji ili kuzuia mafuriko ya kila mwaka barabarani.

Picha|Kevin Odit
Idara ya Utabiri wa Hali ya Hewa nchini tayari imetoa onyo kuwa mvua kubwa itaendelea kunyesha katika sehemu nyingi za Pwani, hali ambayo imezua hofu zaidi ya usumbufu na madhara kwa wakazi.
Katika mahojiano ya awali, Gavana Abdulswamad Nassir alikanusha madai kuwa mafuriko hayo yanasababishwa pekee na kukosa mabomba ya kupitishia maji.
“Kuna maeneo ambako vijiji vimejengwa moja kwa moja juu ya njia za maji. Mvua ikinyesha kupita kiasi, maji hukosa pa kupita, hivyo husababisha mafuriko,” alisema gavana huyo.
Ili kupunguza makali ya mafuriko, serikali ya kaunti imepeleka magari ya kuvuta maji (boozers) kufyonza maji kwenye barabara zilizojaa maji katika maeneo kama Nyali.
Hata hivyo, wakazi wanasema hatua hiyo imechelewa mno.
“Matumizi ya magari ni suluhu ya muda mfupi. Tunahitaji mfumo wa kisasa wa mabomba ambao unaweza kudhibiti mvua kubwa. Tunakumbwa na hali hii kila mwaka, lakini hatua madhubuti hazichukuliwi,” alisema Bw Charles Okoth, mfanyabiashara kutoka Nyali.
Hasara za kiuchumi zinaendelea kuongezeka. Wafanyabiashara katika barabara ya Beach Road wameripoti kupoteza wateja kutokana na kushindwa kufikia maduka yao kutokana na mafuriko.