IEBC: Idadi kubwa ya vijana Mombasa huenda wasipige kura kwa kukosa vitambulisho
IDADI kubwa ya vijana katika Kaunti ya Mombasa huenda wakakosa kupiga kura mwaka ujao kwa kukosa vitambulisho.
Wakati zoezi maalumu la kuwasajili wapiga kura wapya nchini kote likifikia tamati Jumanne, ilibainika kuna maelfu ya wakazi ambao wamehitimu kupiga kura katika Kaunti ya Mombasa lakini hawangeweza kujisajili kwa kuwa hawajapokea vitambulisho vya kitaifa.
Eneobunge la Mvita lilitangazwa kuongoza kwa idadi kubwa ya wapigakura wapya waliosajiliwa kwa muda wa mwezi mmoja uliopita.
Kati ya wapigakura wapya 47,632 waliosajiliwa kufikia Jumanne asubuhi, eneo la Mvita lilisajili wapigakura 16,671 wapya ikifutwa na Changamwe kwa wapigakura 14,289 licha ya changamoto za ukosefu wa vitambulisho kwa waliolengwa kusajiliwa.
Maeneobunge ya Kisauni, Jomvu, Nyali na Likoni yalifuatana, yote yakiwa na idadi chini ya asilimia 25 ya waliolengwa kusajiliwa.
Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) iliomba waliokosa nafasi katika zoezi lililofanyika katika wadi waendelee kujiandikisha kwa ofisi za tume hiyo za kaunti na Huduma Centre.
Hata hivyo, kuafikia idadi hiyo, IEBC ilikuwa imeongeza vituo vya usajili 42 ili kuhudumia ongezeko la idadi ya watu wakati wa zoezi hilo lililoanza Machi 30 na kumalizika Aprili 28.
Kati ya vituo hivyo 42 vipya vya usajili vilivyolenga kuwafikia wapiga kura wapya, Likoni ilikuwa na vituo 17, Kisauni 10, Nyali 5, Changamwe na Jomvu kila moja vituo 4, huku Mvita ikiwa na vituo 2.
Msimamizi wa uchaguzi wa IEBC Kaunti ya Mombasa, Dkt Swalhah Yusuf, alisema jumla ya vituo 269 vya usajili Mombasa vilifanikiwa kusajili asilimia 65 ya idadi iliyolengwa kufikia Aprili 27, siku moja kabla ya zoezi hilo kumalizika.
Alitaja ukosefu wa vitambulisho na kuchelewa kwa vijana kupata vitambulisho kuwa changamoto kuu.
Dkt Yusuf aliwahimiza vijana ambao hawakupata vitambulisho kwa wakati kufika katika Huduma Centre au ofisi za uchaguzi za kaunti kujisajili wakati wowote wa mwaka kabla ya Uchaguzi Mkuu mwaka ujao.
“Tulikuwa na lengo la kusajili wapiga kura wapya 73,280 lakini tulifanikiwa kufikia asilimia 65 siku moja kabla ya zoezi la ECVR kumalizika, sawa na watu 47,632.
“Tulikumbwa na changamoto ya vijana kutopata vitambulisho kwa wakat, lakini tunawaomba wasiwe na wasiwasi kwani ofisi zetu na Huduma Centre zinaendelea kutoa huduma ya usajili wa wapiga kura mwaka mzima,” alisema Dkt Yusuf.
Kwa mujibu wa taarifa kutoka vituo vya usajili wa vitambulisho, Mombasa ilikuwa na vitambulisho 23,137 ambavyo havijachukuliwa katika afisi za Bima Towers, 147 katika Huduma Centre, na karibu vijana 2,100 waliokuwa na stakabadhi za kusubiri vitambulisho.
Kwa mujibu wa meneja huyo wa IEBC, kaunti hiyo ilipokea maombi 9,360 ya uhamisho wa vituo vya kupigia kura huku watu 137 wakirekebisha taarifa zao za kupiga kura.
“Hatukushuhudia tukio lolote la kiusalama, zoezi lilikuwa la mafanikio na makarani pamoja na vifaa vilikuwa salama bila uhalifu wowote kuripotiwa. Tunatumaini hali hiyo itaendelea hadi Uchaguzi Mkuu,” alisema Dkt Yusuf.