Mali ya Ruto hatarini kupigwa mnada kuhusu fidia
NAIBU Mwenyekiti wa Tume ya Huduma za Mahakama (JSC) Isaac Ruto anapambana kortini kuzuia mali yake isipigwe mnada kwa kukosa kulipa fidia ya Sh4 milioni kwenye kesi inayomkabili.
Bw Ruto anatakikana kulipa pesa hizo kwa waziri wa zamani wa Kaunti ya Bomet Elizabeth Langat kwa kutoa matamshi ya kumchafulia jina kuwa hajahitimu kushikilia wadhifa wake mnamo Machi 2016.
Gavana huyo wa zamani wa Bomet aliwasilisha ombi mahakamani mnamo Machi 18 akitaka aruhusiwe kulipa fidia hiyo lakini kwa kutoa Sh100,000 kila mwezi.
Bw Ruto aliwasilisha ombi hilo baada ya kupoteza rufaa ambayo alikuwa amewasilisha kupinga uamuzi uliotolewa mnamo 2020 uliompata na hatia.
Akiwa Gavana wa Bomet, Bw Ruto aliyatoa matamshi hayo wakati wa kikao na wanahabari ambacho alitangaza kuwa alimfuta Bi Langat kazi kutoka kwa Baraza lake la mawaziri.
Habari hizo zilichapishwa na gazeti moja nchini bila Bi Langat kupewa nafasi ya kujitetea. Hapo ndipo Bi Langat aliwasilisha kesi mahakamani dhidi ya Bw Ruto na pia gazeti hilo mnamo 2017.
Kwenye uamuzi wake 2020, mahakama ilimpata Bw Ruto na gazeti hilo na hatia ambapo walitakiwa kulipa fidia ya Sh5 milioni.
Baada ya rufaa, mahakama iliamua Bw Ruto alipe asimia 70 ya hela hizo nao usimamizi wa gazeti hilo asilimia 30.
Kortini, Bw Ruto anasema pesa hizo ni nyingi sana na kuwa hawezi kuzilipa. Hii ina maana kuwa iwapo uamuzi huo utatekelezwa basi ataanikwa zaidi au kukodolewa macho na hasara ya kifedha.