Atwoli ataka wafanyakazi waongezwe mishahara kwa asilimia 23 Leba Dei
ROHO imeanza kuwadunda wafanyakazi wakiuliza iwapo watapata nyongeza ya mishahara Leba Dei mnamo Mei 1.
Hii ni baada ya kuibuka kuwa Muungano wa Vyama vya Wafanyakazi Nchini (COTU) unaendelea na mazungumzo ya kuhakikisha wanapewa nyongeza ya asilimia 23 ya mishahara.
Katibu Mkuu wa Cotu Francis Atwoli alisema kuwa anaendelea na mazungumzo ya kuhakikisha wafanyakazi wanakingwa dhidi ya kupanda kwa gharama ya maisha, hasa kufuatia ongezeko la bei ya mafuta ambalo limepandisha gharama za usafiri, chakula na bidhaa nyingine muhimu.
“Iwapo bei ya mafuta na bidhaa za petroli itaongezeka, sisi kama wawakilishi wa wafanyakazi hatuna budi ila kujadiliana ili kupata mishahara bora. Hilo ndilo tunalofanya sasa na tuna matumaini kuwa Rais atatangaza nyongeza ya mishahara wakati wa Siku ya Wafanyakazi mwaka huu,” akasema katibu huyo mkongwe wa Cotu.
Aliongeza kuwa vyama vya wafanyakazi tayari vinaendeleza mazungumzo ya kuboresha mishahara huku vingine vikiangazia upya Mikataba ya Makubaliano (CBA) ili kuioanisha na hali halisi ya kiuchumi.
“Tumejadiliana kuhusu nyongeza ya mishahara, na baadhi ya vyama vinaendelea kupitia upya mikataba yao ili kuwakinga wafanyakazi dhidi ya mfumko wa kiuchumi inayosababishwa na bei ya mafuta. Tunatoa wito wa nyongeza ya asilimia 23 ya mishahara katika Siku ya Leba,” akaongeza.
Nyongeza ya juu ya mshahara ambayo Cotu imewahi kujadiliana na serikali ni asilimia 23.4 mnamo 2022.
Aidha, Bw Atwoli alitoa wito wa siasa komavu nchini, akionya kuwa misukosuko ya kisiasa inaweza kuhatarisha maisha ya wafanyakazi.
Alisema mvutano wa kisiasa unaweza kulemaza uthabiti wa kiuchumi na hatimaye kuwaathiri zaidi wafanyakazi, wanawake na watoto.
“Siasa ndizo hujenga au kuharibu taifa na nchi hii ikianguka, wafanyakazi, wanawake na watoto ndio wataathirika zaidi. Hatuwezi kusimama kando huku siasa zikivuruga uthabiti unaolinda ajira za wafanyakazi,” akasema.
Aliwataka wafanyakazi waepuka kuunga mkono wito wa maandamano bila kuusaili kwa undani , akiwahimiza kujiuliza iwapo hatua hizo zinanufaisha maslahi yao.
“Kila mara unaposikia mwanasiasa akihamasisha maandamano, lazima tujiulize kama wafanyakazi maandamano hayo yanatusaidia kivipi? Hatuwezi kuandamana kwa masuala yaliyo nje ya uwezo wa serikali ya Kenya,” akasema.