Habari

Mpango wa kutambua ujuzi wa wanajuakali kirasmi ulivyozimika

April 20th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MAPEMA mwaka 2024, serikali ilisherehekea mafanikio makubwa baada ya wafanyakazi 601 kutoka kundi la majaribio kupatiwa vyeti chini ya mpango wa Kutambua Ujuzi (RPL).

Hafla hiyo ilionekana kama ishara ya mwelekeo mpya. Kilichofuata hakikuwa hivyo.

Kilichofichwa katika sherehe hizo ni kwamba miundombinu ya kuendesha mpango huo ikiwemo wathibitishaji ujuzi, mifumo ya viwango vya kitaaluma na taratibu za utekelezaji bado ilikuwa inaandaliwa.

Wataalamu wa RPL nchini kote walikuwa, na bado baadhi yao wangali wanapokea mafunzo.

Mifumo ya vyeti vinavyotarajiwa kusaidia zaidi wafanyakazi wa sekta isiyo rasmi (jua kali), haikuwa imekamilika.

Kwa maneno mengine, mpango ulitangazwa kabla haujawa tayari kutekelezwa.

Bw Stephen Njenga, mtaalamu wa RPL katika taasisi moja kubwa ya mafunzo ya ufundi mjini Thika, amesema ameshuhudia idadi ya wanaojiunga ikishuka hatua kwa hatua.

“Wastani wetu wa kila mwezi ni wanafunzi 10. Tulianza na zaidi ya 220, lakini hadi sasa ni 84 tu wanaosubiri vyeti. Wale tuliowafanyia tathmini mwezi Oktoba bado hawajapata vyeti. Hii inawafanya wengi kusita kuendelea. Kila tunapokwenda kufanya tathmini, watu huuliza ‘nini hatima ya wale wa Oktoba?’ Hata sisi inatufanya turudi nyuma kidogo,” alisema.

Godana, 43, fundi kutoka Kaunti ya Wajir, alisafiri hadi Thika kutafuta uthibitisho wa ujuzi wake kupitia RPL.

Alisema chaguo lake lilikuwa finyu kutokana na upungufu wa vituo vilivyoidhinishwa nyumbani kwake.

“Ninatoka Wajir. Hakuna fursa nyingi za elimu na ajira. Kulikuwa na kituo kimoja tu kilichoidhinishwa. Nilikuja hapa kujaribu bahati yangu. Nilipofika, walinishauri niweze kulipa angalau Sh25,000 kufidia mapungufu ya ujuzi kabla ya tathmini. Sikuwa na uwezo, nikajitoa kabisa,” alisema.

Ada rasmi ya RPL ni kati ya Sh3,000 hadi Sh5,500, ikiwa ni gharama iliyoundwa kuwa nafuu ili kufungua milango kwa wale waliokosa elimu rasmi.

Hata hivyo, ndani ya taasisi zinazotekeleza mpango huo, hali ni tofauti.

Bw Njenga alisema vifaa vya tathmini hutumika mara moja tu na kutupwa na hakuna bajeti ya kuvibadilisha.

Ada rasmi haitoshi kugharamia gharama halisi za tathmini, hivyo taasisi hulazimika kuziba pengo hilo.

“Wafanyakazi wengi wa jua kali ni wa mikataba ya siku. Hawana ajira ya uhakika. Siku ya kufanya tathmini wanapoteza kipato. Ukikosa kazi siku hiyo, hujui kesho utakula nini,” aliongeza.

Mpango huo pia haujaweka posho kwa wanaofanya mitihani wala fidia ya kipato kinachopotea. Hii inafanya iwe vigumu kwa walengwa wake wakuu kushiriki.

Kwa mujibu wa muundo wake, RPL inaruhusu tathmini kufanyika kwenye mazingira ya kazi ya anayetuma maombi.

Hata hivyo, kwa vitendo, mfumo huo ni dhaifu. Mthibitishaji hulazimika kusafiri kwenda eneo la kazi baada ya nafasi kuwekwa.

Lakini wafanyakazi wa vibarua hawana udhibiti wa ratiba zao.

Wakati mwingine tathmini huahirishwa kwa sababu mfanyakazi hakupata kazi siku hiyo au amepangiwa kazi tofauti na ile inayotathminiwa.

Bw Peter Njihia, Mratibu wa RPL katika Mamlaka ya Mafunzo ya Viwanda (NITA), alikiri changamoto za utekelezaji.

“NITA kupitia mpango wa NYOTA na njia nyingine imeweza kusajili takriban watu 200,000, ingawa bado hatujafikia lengo la 420,000 kwa mwaka wa kifedha. Tuko kwenye mchakato wa kuboresha mitaala ili iendane zaidi na wafanyakazi wa sekta isiyo rasmi,” alisema.