Vigogo wa Meru sasa wasaka maridhiano na Kawira
BAADHI ya viongozi kutoka Kaunti ya Meru waliohusika katika kumbandua gavana wa zamani Kawira Mwangaza mamlakani, sasa wanasaka kuridhiana naye kuelekea uchaguzi huo.
Viongozi hao ni Waziri wa zamani wa Kilimo Mithika Linturu, Gavana wa zamani Kiraitu Murung’i na Mbunge wa Tigania Mashariki Mpuru Aburi.
Bi Mwangaza alipoteza kiti chake kutokana na hoja ya kumtimua katika Bunge la Kaunti ya Meru na madiwani. Bw Murungi, Munya, Linturi na wengine waliwaunga madiwani kwenye hoja hiyo ya kumtimua Bi Mwangaza.
Bw Murungi mwenyewe mnamo Machi alikiri kuwa alikuwa kati ya wanasiasa, wazee na viongozi wa kidini waliopanga njama ya kuondolewa kwa Bi Mwangaza afisini.
Akizungumza Ijumaa wiki jana wakati wa mazishi ya mwanawe Anita Kendi, Bw Murungi alijuta kwa kugeuza uhasama wa kisiasa kuwa tofauti za kibinafsi.
“Kifo cha mwanangu kimefanya ninyenyekee, kuanzia leo, hutaniona nikiwatusi wanasiasa wengine. Watu wengi ambao sikuwatarajia wamekuja kutuambia pole, nilishangaa sana kumwona Gavana Kawira Mwangaza nyumbani kwangu,” akasema.
“Amefanya nigundue mazuri ya ubinadamu. Kuanzia leo sitampuuza yeyote,” akaongeza. Bw Aburi ambaye alikuwa na uhasama mkubwa na Bi Mwangaza ameghairi nia na kusema kuwa atakuwa rafikiye.
“Nilifanya kampeni kali ili Peter Munya asichaguliwe mnamo 2017 na baadaye tukawa marafiki. Pia nilimpinga Kiraitu Murungi 2022 na leo tunaongea. Nitafanya hivyo kwa Kawira,” akasema wakati wa ibada ya kanisa kule Kiirua mnamo Jumapili.
“Kuna chochote kibaya nikitatua tofauti kati yangu na Kawira Mwangaza ? Msishangae hivi karibuni tutasalimiana naye,” akasema.
Licha ya kuondolewa kwake, Bi Mwangaza ana uungwaji mkono nyanjani na hivi majuzi alijiunga na mrengo wa Linda Mwananchi inayoongozwa na Katibu Mkuu Edwin Sifuna.