Rais Ruto aimarishiwa usalama kwenye mikutano huku akikamilisha ziara Pwani
USALAMA jana uliimarishwa katika mikutano ya Rais William Ruto eneo la Pwani, siku moja baada ya kijana kumfikia jukwaani bila kuzuiwa na walinzi wake.
Tukio hilo lilifanya Naibu Inspekta Jenerali wa Polisi Eliud Lagat kufanyia mageuzi kikosi cha walinzi wa Rais mnamo Jumapili jioni.
Rais alifikiwa na mwanaume aliyekuwa amebeba bibilia wakati wa hafla ya shukrani Bamba Kaunti ya Kilifi. Hafla hiyo iliandaliwa na Katibu katika Wizara ya Masuala ya Vijana Fikirini Jacobs.
Hata hivyo, hali ilikuwa tofauti jana kiongozi wa nchi alipokuwa akitamatisha ziara yake Pwani hapo jana.
Polisi walikuwa kila mahali, wengine wakiwa wamevaa kiraia na pia kikosi hatari cha Recce kilionekana katika mikutano yake.
Katika eneo la Majengo, Mombasa, Rais Ruto alionekana mtulivu akisalimiana na wakazi.
Kwa wakati mmoja hata alisimama ili kumbeba mtoto aliyekabidhiwa kwake na mmoja wa wafuasi wake.
Hata hivyo, maafisa wake wa usalama waliweka ulinzi mkali kumzunguka, wakizuia umma kumkaribia.
Baadhi ya shughuli zilizokuwa zimepangwa Nyali, Kaunti ya Mombasa, na Kaptuk huko Mariakani nazo zilifutwa kutokana na kile duru za kuaminika ni kwa sababu za kiusalama.
Wakati huo huo mwanaume ambaye alimfikia Rais kule Bamba bado hajulikani aliko japo duru ziliarifu alistahili kufikishwa mahakamani kule Kilifi.
Aidha, utambulisho wake haujajulikana na kufikia saa 11 jana jioni hakuwa amefikishwa kortini.
Vilevile duru nyingine ziliarifu kuwa kijana huyo alikuwa mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Pwani katika Kaunti ya Kilifi.
Hata hivyo, wanafunzi wachache waliokuwa chuoni humo, ambacho kimefungwa kwa likizo ndefu, walisema hawamfahamu.
Baada ya kumaliza mkutano wake kule Bamba, Rais aliwashauri walinzi wake wasimdhuru mwanaume huyo japo tukio hilo lilichangia kuondolewa kwa afisi mkuu anayehusika na ulinzi wa rais Noah Kirwa Maiyo.