Habari za Kitaifa

Afueni kwa jamaa na marafiki dereva wa teksi Victoria Mumbua akipatikana hai

Na KEVIN MUTAI September 30th, 2024 Kusoma ni dakika: 1

DEREVA wa teksi mjini Mombasa aliyeripotiwa kutoweka amepatikana akiwa hai, karibu na bwawa la Uriri, Kaunti ya Migori.

Kulingana na Msemaji wa Polisi Resila Onyango, Victoria Mumbua Muloki, 35, alipatikana akiwa hali mahututi na inaaminika alitupwa huko na waliomteka nyara.

“Tulimpata akiwa amepoteza fahamu, ana majeraha kwenye kichwa na mikono. Yumo hali mbaya na tunafanya mipango ya kumsafirisha hadi Mombasa kwa matibabu bora,” akasema Bi Onyango.

Bi Mumbua alitoweka Ijumaa baada ya kumpeleka mteja eneo la Samburu, Kwale, kutoka Mombasa.

Wakizungumza na Taifa Leo, familia yake ilisema wanajiandaa kwenda kumpokea katika uwanja wa ndege wa Moi.

“Nina furaha kuhusu habari hizi na nashukuru Mungu kwamba nitamuona binti yangu tena,” akasema mamake, Anne Kanini.

Idara ya upelelezi DCI awali ilikuwa imetuma wachunguzi kutoka Mombasa kwenda Nakuru kumhoji mshukiwa mmoja aliyepatika na gari la Bi Mumbua Nakuru.