Habari za Kitaifa

Bilionea Aliko Dangote awazia kujenga kiwanda cha kusafisha mafuta Kenya

Na REUTERS May 10th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

BILIONEA wa Nigeria Aliko Dangote anatathmini kujenga kiwanda cha kusafisha mafuta chenye uwezo wa kuchakata mapipa 650,000 kwa siku hapa nchini.

Kulingana na taarifa ya gazeti la Financial Times iliyochapishwa Jumapili, bwenyenye huyo analenga kufanya hivyo ili kuinua uchumi wa Afrika Mashariki. “Nalenga zaidi Mombasa kwa sababu ina bandari kubwa zaidi na yenye kina kirefu,” akasema Dangote katika mahojiano na FT.

Taarifa hiyo inatokea mwezi mmoja baada ya Rais William Ruto kusema kuwa nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) zilikuwa kwenye mazungumzo kuhusu mpango wa kujenga kiwanda cha pamoja cha kusafisha mafuta katika Bandari ya Tanga, Tanzania.

Kiwanda anacholenga Dangote kitakuwa sawa na kile ambacho amekijenga kwao Nigeria.

Akilinganisha bandari ya Mombasa na ile ya Tanga, Dangote alipendelea Kenya akisema ni pazuri zaidi kutokana na ukubwa wa uchumi wake na kiwango cha juu cha matumizi ya bidhaa za mafuta.

“Wakenya hutumia mafuta zaidi na uchumi wake ni mkubwa zaidi,” akasema.

Ingawa hivyo, tajiri huyo alisema kuwa hatua itakayofuata sasa iko mikononi mwa Rais Ruto.

“Mwelekeo sasa utatoka kwa Rais Ruto. Chochote ambacho Rais Ruto atasema ndicho nitakachofanya,” alisema akisisitiza ushirikiano lazima utoke kwa nchi za EAC.

Kulingana na taarifa za Financial Times, Dangote anakadiria kuwa itagharimu kati ya dola bilioni 15 (Sh1.9 trilioni) hadi 17 (Sh2.1 trilioni) kujenga kiwanda hicho cha kusafisha mafuta.

Kwa sasa, nchi za Afrika Mashariki huagiza bidhaa zote za mafuta yaliyosafishwa kutoka nje, hasa kutoka Mashariki ya Kati.

Nchi za EAC ni kati ya zile zilizokumbwa na uhaba wa mafuta wakati vita vilikuwa vikiendelea kati ya Amerika-Israel dhidi ya Iran.