Pensheni: Vitisho baridi dhidi ya Uhuru
KAULI za baadhi ya viongozi wa Kenya Kwanza kutaka marupurupu ya rais mstaafu Uhuru Kenyatta yapunguzwe au yaondolewe zimeendelea kuzua mjadala mkali, huku wakosoaji wakionya dhidi ya kutumia sheria kama silaha ya kisiasa.
Seneta wa Nandi Samson Cherargei, ambaye ni mshirika wa Rais William Ruto, alipendekeza Uhuru apokonywe marupurupu hayo kwa kuendelea kushiriki siasa kinyume cha sheria baada ya kustaafu.
Hata hivyo, pendekezo hilo lilipuuzwa na wandani wa Rais Ruto pamoja na wataalamu wa Katiba wakisema ni siasa za pesa nane.
Mbunge wa Belgut Nelson Koech, ambaye ni mwandani wa karibu wa kiongozi wa nchi, alimtetea Uhuru, akisema viongozi wanapaswa kuheshimu Katiba na haki zinazotolewa kwa marais wastaafu.
Akizungumza katika mazishi kijijini Chemororoch, Kaunti ya Kericho, Koech alipinga vikali mjadala kuhusu kuondolewa kwa marupurupu ya rais huyo wa nne wa Kenya.
“Wachana na hii mambo kidogo kidogo, mambo ambayo haisaidii. Kumwandama Uhuru Kenyatta, kwa nini tufanye hivyo. Sasa marupurupu ya mtu ambayo yako kwa katiba unasemaje yatatolewa?” akahoji.
Alisisitiza kuwa marupurupu ya rais mstaafu yamelindwa kikatiba na hayapaswi kutumiwa kama njia ya kulipiza kisasi cha kisiasa viongozi wanapotofautiana.
Koech pia aliwataka viongozi kuwa waadilifu na kuwatendea wengine jinsi wanavyotaka kutendewa siku zijazo watakapostaafu mamlakani.
“Tuwatendee wengine tunavyotaka kutendewa pia. Wacha Uhuru aende na zake,” alisema.
Kauli zake zilijiri wakati ambapo baadhi ya viongozi wa kisiasa wamekuwa wakitaka marupurupu ya marais wastaafu yapitiwe upya, hasa kufuatia mvutano wa kisiasa kati ya Uhuru na utawala wa Kenya Kwanza.
Cherargei amepeleka hoja Seneti akitaka marupurupu ya Uhuru yasitishwe au yapunguzwe.
Alisema rais huyo mstaafu hawezi kuendelea kufaidika na fedha za umma huku akiendelea kushiriki siasa kama kiongozi wa chama cha Jubilee.
Katika hoja yake, Cherargei anataka fedha zitakazookolewa kutokana na kupunguzwa kwa marupurupu hayo zielekezwe kwa maendeleo ya wananchi.
Lakini hoja hiyo imepingwa vikali na baadhi ya viongozi wa upinzani na hata baadhi ya wabunge wanaounga serikali.
Mbunge wa Rarieda Otiende Amollo alisema mjadala huo ni “kupoteza muda,” akieleza kuwa Katiba inalinda marupurupu ya rais mstaafu chini ya Kifungu cha 151(3).
“Mijadala mingine ni kupoteza muda. Hoja hii ya Seneta Cherargei haina msingi. Marupurupu ya rais mstaafu hayawezi kubadilishwa akiwa hai. Tulihakikisha hilo linawekwa kwenye Katiba.”
Mvutano huo uliongezeka baada ya Uhuru kutoa hotuba kupitia simu ya ndugu yake Muhoho Kenyatta, ambapo alimshutumu Rais Ruto kwa kujaribu kumzima kisiasa.
Uhuru alisema ana haki ya kutetea chama chake kama wafanyavyo viongozi wengine wa dunia hata baada ya kustaafu. Rais huyo mstaafu aliapa kuwa hatafumbwa mdomo na yeyote.
Wadadisi wa siasa wanahoji kwamba hatua ya Cherargei ni baridi sana japo wanasisitiza katika siasa hakuna la kupuuzwa.
“Hata kiti cha naibu rais kilionekana kuwa kimelindwa katika katiba hadi alipotofautiana na rais na akaondolewa. Hata hivyo, vitisho vya kuvua Uhuru posho lake kama rais mstaafu ni baridi,” asema mchanganuzi Peter Katana.