Habari za Kitaifa

Gachagua: Kindiki akae tu kwa kiti, sikitaki tena — lakini mnilipe

Na JOSEPH WANGUI April 28th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

ALIYEKUWA Naibu Rais Rigathi Gachagua sasa ameachana na nia ya kutaka arejeshewe wadhifa wa unaibu rais akimakinikia malipo ya huduma alizotoa katika afisi hiyo kabla ya kuondolewa madarakani mnamo Oktoba 2024.

Kwenye kesi aliyowasilisha mahakamani kupinga kubanduliwa kwake, Bw Gachagua Aprili 27, 2026 alibadili ombi lake na kusema kuwa sasa anamakinikia fidia pamoja na malipo ya kustaafu.

Mawakili wake sasa wanalenga kupambana kuhakikisha kuwa korti inatoa donge nono kwake licha ya kuondoka afisini karibu mwaka moja na nusu uliopita.

Chini ya Sheria za Malipo ya Kustaafu, Naibu Rais hulipwa asilimia 80 ya mshahara aliolipwa mara ya mwisho pamoja na pesa za jumla ambazo zinatokana na mshahara wa mwaka mmoja kwa kila mwaka aliohudumu.

Naibu Rais hulipwa Sh1.2 milioni kila mwezi ambapo mshahara ni Sh736,313, marupurupu ya nyumba Sh300,000 pamoja na marupurupu mengine.

Pia hupewa magari mawili na gari moja lenye magarudumu manne makubwa ambayo hubadilishwa kila baada ya miaka minne.

Pia anapewa marupurupu ya mafuta ambayo ni asilimia 15 ya mshahara wake. Manufaa mengine ni bima bora ya matibabu kwake na familia yake, wafanyakazi, pasipoti kwake na mkewe, kutumia eneo la wageni mashuhuri kwenye viwanja vya ndege pamoja na kupewa walinzi akiwahitaji.

Mbele ya Jopo la Majaji watatu Erick Ogolla, Anthony Mrima na Frida Mugambi, mawakili wa Bw Gachagua kwa kesi yao hailengi kumakinikia mchakato wa kuondolewa kwa mteja wao bali fidia kwa kile walichosema ni kuondolewa afisini kinyume cha sheria.

Wakili Paul Muite anayeongoza jopo la majaji wa Bw Gachagua alisema kuwa mteja wao aliondoa ombi la kutaka arejeshewe wadhifa wake na sasa analenga fidia.

“Mwasilishaji wa kesi ameondoa ombi la kurejeshwa kama naibu rais,” akasema Bw Muite katika Mahakama ya Milimani, Nairobi.

Aliongeza kuwa sasa wanalenga kuhakikisha kuwa mahakama inatoa uamuzi kuwa mchakato wa kutimuliwa kwa Bw Gachagua haukufuata sheria ili aliyekuwa naibu rais alipwe mshahara wake na marupurupu ambayo mshikilizi wa wadhifa wa naibu rais anastahili kutoka 2022-2025.

Kando na mshahara, wanataka marupurupu ya kustaafu kutoka kwa afisi hiyo pamoja na marupurupu mengine.

Bw Muite sasa amesawiri kesi hiyo kama yenye malengo ya kupata hela badala ya ushindani wa kisiasa jinsi ulivyokuwa mwanzoni alipotimuliwa.

Anadai kesi hiyo iliharakishwa kwenye Bunge la Kitaifa na Seneti na haikufikia viwango vya kikatiba.

“Hakukuwa na ushirikishaji wa maana wa umma na ule uliofanyika haukuwapa raia nafasi ya kusikiza upande wa Bw Gachagua,” akasema akisisitiza umma uliwasilishiwa na madai kutoka Bunge la Kitaufa na si upande wa Bw Gachagua.

Aliyekuwa naibu rais alihudhuria kikao hicho cha kesi akiwa ameandamana na mkewe Dorcas na wandani wake wa kisiasa, huku mawakili wake wakiunganisha kesi zote ambazo zilipinga kutimuliwa kwake mnamo 2024.

Hasa walishangaa kwa nini seneti na bunge la kitaifa waliendeleza vikao vyao hadi usiku ilha muda wa kufanya kazi kwa kawaida kwao ni mchana.

Aliongeza kuwa mkutano wa ushirikishaji wa umma uliofanyika kwenye Ukumbi wa Bomas uliongozwa na baadhi ya wabunge wa ODM kutoka Kaunti ya Nairobi.

Wakili Elisha Ongoya naye alisema mchakato wa kumwondoa Bw Gachagua haukufuata sheria na ulikuwa umeshaamuliwa.

“Mchakato huo ulifanyika tu ilhali ukweli ni kuwa hatima ya Bw Gachagua ilikuwa ishaamuliwa,” akasema Bw Ongoya.

Aidha wakili huyo alisema kuwa kauli ya ‘serikali ya hisa’ haikustahili kutumika kumwaadhibu Bw Gachagua kwa sababu ipo kwenye mkataba wa kugawana mamlaka Muungano wa Kenya Kwanza.

Wakili Dudley Ochiel naye alifafanua kuwa Seneti ilikosa kufuata katiba na haikuteua kamati maalum ya kuchunguza madai dhidi ya Bw Gachagua akisema naibu huyo wa rais hakusikizwa.

Wakili Tom Macharia naye akimtetea aliyekuwa naibu rais, alisema masaibu yake yalianza wakati wa maandamano ya Gen Z mnamo Juni 2024.

Alidai kuwa masaibu ya Bw Gachagua yalianza aliposhutumu Shirika la Ujasusi na vyombo vingine vya usalama kutokana na jinsi vilivyoshughulikia maandamano hayo.

Kesi hiyo itaendelea kusikizwa Mei 7.