Kindiki ajipange? Ndoto ya Joho kuwa naibu wa Ruto yapigwa jeki
VIONGOZI wakuu katika Chama cha ODM wamekubaliana na wanasiasa wanaomtaka Waziri wa Madini na Uchumi wa Baharini, Bw Hassan Joho, kuwa mgombea mwenza wa Rais William Ruto katika Uchaguzi Mkuu ujao.
Hatua hiyo imejiri siku chache baada ODM na UDA kutangaza mwelekeo kuhusu mazungumzo ya muungano wa kisiasa kabla uchaguzi mkuu ujao ufanyike.
Mwenyekiti wa Kitaifa wa ODM, Bi Gladys Wanga, alisema Bw Joho anatosha kuwa mgombea mwenza wa Rais Ruto kutokana na ushawishi wake wa kisiasa.
Bi Wanga, alisema ODM itamuunga mkono Bw Joho, kuwa Naibu Rais.
Magavana Gideon Mung’aro, Paul Otuoma, Abdulswamad Nassir na Simba Arati wote walisisitiza umuhimu wa ODM kuimarisha ngome zake na kuunga mkono azma ya Bw Joho.
Bi Wanga ambaye pia ni Gavana wa Homa Bay aliwahakikishia wanachama wa ODM kuwa chama kinatarajia kupata asilimia 50 ya nafasi za serikali iwapo Rais Ruto atachaguliwa tena kwa awamu ya pili ya uongozi.
Alisema mazungumzo yanayotarajiwa ni kuhusu kugawana mamlaka.
“Chochote kitakachowekwa mezani, tutachukua asilimia 50 wabakie na asilimia 50. Wakichukua urais, ODM itachukua naibu rais. Tukishapata, tutajadili kama Bw Joho anatosha au hatoshi. Tutagawana nafasi na kama chama tutapata wizara kadhaa,” alisema Bi Wanga, kwenye mkutano wa hadhara Jumapili katika Kaunti ya Kilifi.
Hata hivyo aliwasihi Wapwani kuendelea kuunga mkono chama cha ODM ili wanufaike zaidi.
Bi Wanga alisema vijana na wale wanaoishi na ulemavu wana nafasi katika chama cha ODM ambacho alisema hakina ubaguzi wala ukabila.
Kuungwa mkono kwa Waziri Joho, kunafufua azma yake ya kushiriki zaidi siasa za kitaifa ambapo alishatangaza kwua atawania Urais 2032 baada ya Rais Ruto kumaliza mihula yake miwili.
Ushawishi wa Waziri Joho katika siasa za Pwani, utajiri na umaarufu wake nchini umemsaidia kupata ungwaji mkono katika siasa za kitaifa.
Kando na kujihusisha kwenye biashara ya mabilioni ya pesa, Bw Joho pia amekuwa kwenye siasa kwa muda mrefu ikiwemo kuwa mbunge wa Kisauni, Naibu Waziri, na Gavana wa Mombasa kwa mihula miwili.
Bi Wanga aliwahimiza viongozi wa ODM Pwani kuhakikisha chama kinasimamisha wagombea katika kila kiti kwanzia, diwani hadi useneta katika kaunti zote sita za eneo hilo.
“Hakikisheni tunashinda viti vyote vya kisiasa katika kaunti sita zilizoko hapa Pwani. Msiruhusu vyama vingine kuingia katika ngome yetu,” alisema.
Wiki iliyopita, Rais Ruto aliongoza kikao cha pamoja kati ya vyama vya UDA na ODM katika Ikulu, ya Nairobi, kilichohudhuriwa na viongozi wakuu wa vyama vyote.
Kikao hicho walikubaliana kwamba Magavana Bi Wanga na mwenzake wa Embu Bi Cecily Mbarire waendelee na mashauriano ya mara kwa mara kabla mazungumzo.
Bi Wanga pia alimkosoa kinara wa chama cha DCP Bw Rigathi Gachagua kwa kauli zake kuhusu marehemu Raila Odinga, akisisitiza ODM haitashirikiana na chama chake.
Bw Joho alisema yuko tayari kwa siasa za kitaifa. Alisema hatokubali chochote chini ya kuchukua mamlaka ya uongozi wa nchi hii kwenye uchaguzi mkuu wa 2032.
“Pwani itazaa Rais. Kama si mimi basi ni mimi,” alisema.