Habari za Kitaifa

Ruto atumia ‘tamtam’ Gusii kukabili ushawishi wa Matiang’i

Na RUTH MBULA, JUSTUS OCHIENG’ April 15th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

RAIS William Ruto sasa analenga kutumia miradi ya mabilioni kumaliza ushawishi wa aliyekuwa Waziri wa Usalama wa Ndani Dkt Fred Matiangí eneo la Gusii.

Kiongozi wa nchi leo anamaliza ziara yake ya siku nne eneo hilo ambapo amekuwa akifungua miradi na kurai eneo hilo limuunge mkono mnamo 2027.

Amekuwa akizindua miradi ya maji, masoko, ujenzi wa nyumba za gharama nafuu, makazi ya wanafunzi wa vyuo vikuu na taasisi za masomo.

Ziara hiyo imesheheni miradi mingi na hasa imejikita katika kuimarisha miundomsingi ya eneo hilo.

“Sitashiriki kampeni ya matusi wakati huu uchaguzi unakaribia na iwapo wapinzani wangu wataamua kuchukua mwelekeo huo, nitawajibu kupitia miradi ya maendeleo,” akasema Rais Ruto kwenye matamshi yaliyoonekana kuwalenga Dkt Matiangí na aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua.

Wachanganuzi wa masuala ya kisiasa wanasema iwapo miradi aliyoizindua Rais Ruto itatekelezwa, basi itakuwa vigumu sana kuzima ushawishi wake eneo hilo hata iwapo Dkt Matiangí ataendelea kuegemea mrengo wa upinzani.

Wakati wa ziara yake Kaunti ya Kisii, aliweka jiwe la msingi la ujenzi wa makazi ya wanafunzi katika Chuo cha Mafunzo ya Kimatibabu ya Nyamache, soko la kisasa la Mogonga na pia masoko mengine 22 ambayo yatajengwa kwa kima cha Sh2.5 bilioni.

Kule Nyakoe eneobunge la Kitutu Kusini, kuna ujenzi wa soko la kisasa unaoendelea ambalo litawahudumia zaidi ya wafanyabiashara 300 na pia kutakuwa na soko lingine kama hilo Kegogi.

“Lengo letu ni kuunganisha nchi huku tukitekeleza miradi ambayo itayabadilisha maisha ya raia. Ndani ya Serikali Jumuishi tunashauriana na viongozi waliochaguliwa na wale wa nyanjani,” akaongeza Rais alipokutana na zaidi ya viongozi 2,000 katika ikulu ndogo ya Kisii.

Pia alizindua ujenzi wa barabara ya Bobaracho-Tingá ambayo ni njia ya kuelekea Kiwanda cha Majanichai cha Gianchore.

Katika Kaunti ya Nyamira, alizindua ujenzi wa barabara ya kilomita 61 katika barabara ya Eronge-Kebuse-Omonyenya ambayo utekelezaji wake umefikia asilimia 58 ukamilike. Barabara nyingine ni Keumbu-Kiendeke na Chabera-Nyamusi-Nyamaiya.

Pia aliweka jiwe la msingi la makazi ya wanafunzi katika Chuo Kikuu cha Nyamira kwa kima cha Sh300 milioni. Serikali pia itatumia Sh500 milioni kujenga Chuo Kikuu cha Nyamira.

Miradi mingine ni ukarabati wa uga wa Gusii kwa kima cha Sh1 bilioni, kupandishwa hadhi kwa Hospitali ya Kaunti ya Nyamira kwa Sh1 bilioni na nyumba 580 za wanafunzi kwenye Chuo cha Mafunzo cha Kimatibabu cha Nyamira.

“Kwa Rais, jibu ni kuanzisha miradi ambayo itasaidia kubadilisha maisha ya watu na apate kura. Hiyo ndiyo maana anazindua ujenzi wa barabara, masoko, vituo vya afya na kuwekeza pia kwenye sekta ya elimu,” akasema Mchanganuzi wa Masuala ya Kisiasa Dismas Mokua.

Viongozi wa kisiasa Kisii nao wamegawanyika kuhusu uungwaji mkono wa Rais na Dkt Matiangí ambaye pia ni naibu kiongozi wa Jubilee.