Akili Mali

Apata tija katika kilimo cha miwa kama ‘tunda’ la kutafuna na kukamua juisi

Na WYCLIFFE NYABERI April 29th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

WADI za Ibeno na Keumbu katika eneobunge la Nyaribari Chache, Kaunti ya Kisii ni maarufu sana katika ukuzaji wa miwa ya kutafuna.

Unapozuru maeneo hayo kwa mara ya kwanza, utakaribishwa na miwa hiyo iliyonawiri katika mashamba ya wakazi wengi ambao wameilima kwa miaka mingi kama kitega uchumi.

Tofauti na miwa inayokuzwa kupelekwa kiwandani kutengeneza sukari, miwa hii ya rangi ya manjano huliwa kama tunda la kuburudisha na kutoa juisi.

Miwa hii ina soko kubwa humu nchini hasa maeneo ya mijini ambapo aghalabu utawaona wachuuzi wakisukuma wilbaro zilizojazwa zao hili wakiichuuza.

Jarida la Akilimali lilimzuru Newton Kennedy, 32, maarufu kama Mzungu kwa jina lingine la lakabu kijijini Mwamaranga, kata ndogo ya Kabosi, Wadi ya Ibeno kujionea fahari ya kilimo hiki na jinsi ya kukifanikisha.

Newton alianza ukulima wa miwa ya manjano mwaka 2020 na anadokeza kuwa alivutiwa na ufanisi aliouona kwa rafikiye ambaye alikuwa ameilima miwa hiyo.

“Nilikuwa nimemzuru mkulima mmoja ambaye ni rafiki yangu na nilipofika kwake, nilikuta watu waliokuja kuinunua miwa yake. Katika kipande kidogo cha ardhi yake, huyo rafiki alinieleza kuwa aliiuza miwa hiyo zaidi ya Sh100,000. Nilivutiwa na pesa hizo nami nikasema kwa kuwa nina shamba, ni lazima ningefanya ukulima huo,” anadokeza.

Alianza kupanda miwa katika shamba la mita 170 kwa 50.

Miwa ikishapandwa, Newton anaeleza kuwa itachukua muda wa miezi 14 kabla ya mkuliwa kuivuna.

Kulingana na mkulima huyu, kilimo cha miwa ya kutafuna kimemletea faida chungu nzima.

“Kabla ya kuanza ukulima huu wa miwa ya njano, sikuwa na ng’ombe lakini sasa hivi, nina ng’ombe wazuri wa maziwa. Pia sikuwa na nyumba nzuri lakini kwa sasa hivi, niko karibu kumaliza nyumba yangu ya matofali na saruji kutokana na kilimo hiki na nihamie huko pamoja na familia yangu,” anafichua.

Mkulima huyu anadokeza kuwa hakuna kilimo chochote kijijini kwao kinachoweza kufikia kilimo cha miwa. Anahoji kuwa tangu aanze kilimo hicho, hajawai vuna au kuuza miwa chini ya Sh150,000.

Anasema miwa inaweza kuvunwa hata mara tatu ikishapandwa kabla ya nguvu zake kuisha.

Hata hivyo, baada ya kuvuna kwa mara ya kwanza, mavuno yatakayofuata yatachukua muda mfupi upatao miezi tisa hivi ikilinganishwa na wakati unapongoja kuvuna kwa mara ya kwanza.

Katika uuzaji wa miwa, Newton anadokeza kuwa wateja wao wengi hutoka jiji la Nairobi. Anasema wanunuzi hao hufurika kila siku kijijini humo kuisaka miwa hiyo ili kuwapelekea wakazi wa mijini.

Anapouza miwa yake, anasema anaweza kuiuza kwa kijumla au akauza mua baada ya mwingine.

“Kwa sasa, mua mmoja bei yake shambani ni Sh23. Shamba langu lina uwezo wa kutoa miwa mizuri hadi 10,000 ikiwa nimefanya kazi ya upanzi na upaliliaji vizuri,” mkulima huyo anaeleza.

Anaeleza kuwa miwa ya kutafuna au manjano inahitaji joto na maji ya kutosha ili kukua.

Udongo wake pia unafaa uwe tifutifu na usiotuamisha maji.

Mzungu anafafanua kuwa mkulima hutumia miwa ambayo haikufikisha uzani wa kwenda sokoni kuzalisha miwa mingine.

Miwa ile inayokataliwa na wanunuzi, hukatwa katwa vipande na kuwekwa katika mitaro iliyolimwa mita moja baada ya mwingine.

Kisha udongo hurudishwa kwa kiasi fulani kufunika mbegu hizo ambazo zitaanza kuota na kuchipuza siku chache tu baada ya kupandwa.

Miwa inapozidi kukua, anahoji kuwa ni sharti mkulima aitunze vizuri ikiwa atataka kupata mazao tele.

“Miwa inapaswa kupaliliwa vizuri na kuwekewa mbolea vizuri. Unapoipanda, unaweza kutumia mbolea asilia lakini inavyozidi kusonga, mbolea za CAN au Urea ni muhimu kwa ukuaji wake,” mkulima huyu anaeleza.

Hata hivyo, Newton anadokeza kuwa ukulima wa miwa ya kutafunwa si jambo rahisi hasa kwa watu wasiokuwa na moyo.

Anaongeza kuwa kadri miwa inavyozidi kukua, inambidi mkulima kuiondolea maganda ndiposa ipate rangi yake ya njano, jambo ambalo si rahisi.

“Kuingia ndani ya miwa si jambo rahisi hasa kunapokuwa na jua. Miwa hiyo huwasha sana na usipokuwa makini, inaweza kukuumiza au hata kukudunga macho kutokana na majani yake yenye ncha kali,” anatahadharisha.