Habari za Kitaifa

Mvua imefika huku, kuweni chonjo, idara yaonya

Na BENSON MATHEKA October 21st, 2025 Kusoma ni dakika: 2

Idara ya Utabiri wa Hali ya Hewa nchini Kenya imewaonya Wakenya wanaoishi katika maeneo mbalimbali ya nchi kujiandaa kwa mvua ya wastani hadi kubwa itakayoanza Jumanne wiki hii hadi Jumatatu wiki ijayo.

Katika utabiri wake wa kila wiki uliochapishwa Jumanne, Oktoba 21, Idara hiyo ilisema kuwa mvua kubwa inatarajiwa kunyesha katika maeneo ya Nyanda za Juu za Kati, Bonde la Ziwa Viktoria, Magharibi mwa Kenya, maeneo ya chini ya Kusini-Mashariki na eneo la Bonde la Ufa.

Katika Nyanda za Juu za Kati, mvua inatarajiwa kunyesha katika kaunti za Nyandarua, Laikipia, Nyeri, Kirinyaga, Murang’a, Kiambu, Meru, Embu, Tharaka Nithi na Nairobi.

Vilevile, katika Bonde la Ziwa Victoria na eneo la Bonde la Ufa, mvua inatarajiwa katika kaunti za Siaya, Kisumu, Homa Bay, Migori, Kisii, Nyamira, Trans Nzoia, Baringo, Uasin Gishu, Elgeyo Marakwet na Nandi.

Kaunti nyingine zinazotarajiwa kupata hali sawa ya mvua ni Nakuru, Narok, Kericho, Bomet, Kakamega, Vihiga, Bungoma, Busia na Pokot Magharibi.

Katika maeneo ya chini ya Kusini-Mashariki, mvua ya wastani hadi kubwa inatarajiwa kunyesha katika kaunti za Kitui, Makueni, Machakos, Kajiado na Taita Taveta, pamoja na maeneo ya ndani ya kaunti ya Tana River.

Idara imewaonya Wakenya wanaoishi katika maeneo yaliyotajwa kuwa waangalifu na kuchukua hatua zinazofaa kutokana na uwezekano wa mafuriko katika kipindi cha mvua siku saba zijazo.

Kulingana na Idara, mvua kubwa inaweza kutokea katika baadhi ya maeneo haya na wakazi wanashauriwa kuwa macho na kuchukua tahadhari zinazostahili.

Utabiri huu unajiri wakati baadhi ya maeneo ya nchi bado yanapitia hali ya joto kali na ukame, hasa katika eneo la Bonde la Ufa, Nyanda za Juu za Kati na maeneo ya chini ya Kusini-Mashariki.

Katika utabiri huo, idara hiyo imetangaza kuwa kuanzia Jumanne, Oktoba 21, viwango vya joto wakati wa mchana katika maeneo ya Pwani, Kaskazini-Mashariki na Kaskazini-Magharibi vitapanda na kuzidi nyuzi joto 30 kiwango cha selsias.

Kaunti zinazotarajiwa kuathiriwa na joto hilo kali ni Mombasa, Kwale, Kilifi, Kitui, Machakos, Makueni, Tana River, Garissa, Isiolo na Mandera.

Utabiri unasema viwango vya joto wakati wa usiku katika Nyanda za Juu za Kati, Bonde la Ufa la Kati na maeneo ya karibu na Mlima Kilimanjaro vinatarajiwa kushuka chini ya nyuzi joto 10 kwa siku saba zijazo.