Dalili ODM kukosa mwaniaji urais 2027 Oburu, Wanga wakitangaza kujerea nyumbani kutetea viti vyao
HUENDA ODM ikakosa mwaniaji wa urais na mgombeaji mwenza kwa mara ya kwanza tangu uchaguzi mkuu wa 2007 katika uchaguzi mkuu ujao.
Hii ni baada ya kiongozi wa chama hicho, Dkt Oburu Oginga, 82 kutangaza kuwa atagombea useneta wa Siaya.
Gavana wa Homa Bay, Gladys Wanga ambaye amekuwa akirindimiwa ngoma ya kuwa mgombea-mwenza wa Rais William Ruto, naye ametangaza kuwa atarejea kuwania muhula wa pili wa ugavana.
Viongozi hawa wawili walikuwa wakiongea jana Kisumu walipokutana na viongozi wanaolenga viti mnamo 2027 kwa kutumia ODM.
“Nina furaha kuwa hapa kama mgombea. Nitatetea kiti changu cha useneta mwaka 2027,” Dkt Oginga alitangaza huku akipigiwa makofi na kushangiliwa wakati wa kutambulishwa kwa wagombeaji wa viti kutoka Kaunti ya Siaya.
Safari ya kisiasa ya Dkt Oginga ilianza zamani.
Aliwahi kuwa diwani wa Kisumu, mbunge wa Bondo, mbunge kwenye wa Bunge la Afrika Mashariki, naibu waziri wa fedha, na sasa ni Seneta wa Kaunti ya Siaya.
Dkt Oginga amekuwa akionyesha uvuguvugu kuhusu hatima yake ya kisiasa tangu achukue usukani mwa ODM baada ya mauti ya marehemu kakake Raila Odinga.
Hasa amekuwa akizungumzia jinsi chama hicho kitashirikiana na kile cha UDA kwenye kura hiyo ya 2027.
Wanasiasa waliohudhuria mkutano wa jana nao walimtaka Dkt Oginga awe mkakamavu hata anapozungumza na UDA, wakisema uungwaji mkono kwa Rais Ruto haufai kuchukuliwa kama jambo la kawaida.
Bi Wanga naye aliunga mkono wito wa kuwa na uteuzi huru, akisema chama lazima kifanye shughuli hiyo kwa njia wazi ikiwa kinataka kuongeza idadi ya viti vyake katika uchaguzi mkuu ujao.
“Tunapaswa kufanya kazi kwa bidii na kupata viti vingi kwenye uchaguzi iwezekanavyo ndiposa lazima tuwe na wagombeaji huru. Tukiharibu uteuzi tutakuwa na tatizo,” akasema.
“Mimi pia ni mgombea, lazima niende mashinani kuwashawishi watu. Hata Oburu ni mgombea na mtu yeyote anaruhusiwa kugombea dhidi yake na wananchi ndio wataamua,” akaongeza.
Bi Emily Awita, Mwenyekiti wa Kamati ya Kitaifa ya Kuratibu Uchaguzi wa ODM, naye alitoa onyo kali dhidi ya utoaji wa hongo kwa maafisa wa chama, akisema jaribio lolote kama hilo litasababisha mwaniaji kupigwa marufuku.
“Msitoe hongo mkitarajia kupata cheti, haviuziwi. Jaribio la kumhonga kamishina yeyote wa kamati ya uchaguzi litakuwa sababu ya kuondolewa kati ya wawaniaji,” akasema Bi Awita.
Aliongeza kuwa tiketi za moja kwa moja zitatolewa tu katika nafasi ambazo zina mgombeaji mmoja pekee.
ODM inatarajiwa kufanya mkutano mkubwa wa hadhara jijini Kisumu mnamo Mei 31, ambapo chama hicho kinatarajiwa kutoa mwelekeo wa kisiasa wa eneo la Luo Nyanza kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027.