Habari za Kitaifa

Ruto alivyofumbia macho kaa moto la mgomo na kuenda ziarani Azerbaijan

Na MWANDISHI WETU May 19th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

KABLA ya Rais William Ruto kuondoka nchini kuelekea Azerbaijan kwa kutumia ndege ya kifahari ya kibinafsi iliyokodishwa Jumamosi, dalili zote ziliashiria kuwa mgomo ulioitishwa na wasafirishaji kote nchini ungelemaza nchi Jumatatu.

Aliondoka pasipo kusema lolote kuhusu janga hilo lililokaribia.

Saa chache baada ya kutua jiji kuu la Baku, Jumapili usiku, maafisa wa miungano inayohusu bidhaa za petroli waliitisha mkutano na vyombo vya habari jijini Nairobi kutangaza kuwa mgomo ungalipo.

Muungano wa Wamiliki Matatu ulijitokeza kwa nguvu zaidi.

Rais Ruto yupo jijini Baku kuhudhuria kongamano la 13 la Warsha ya Maeneo ya Mijini Duniani (WUF) ambapo Kenya ilialikwa kutokana na uongozi na ufanisi wake katika makazi ya bei nafuu na ustawishaji wa maendeleo ya mijini.

Huku mgomo huo ukishika kasi jana asubuhi, tofauti ya Wakenya waliokwama katika vituo vya mabasi au kutembea kazini na ndege ya kifahari aliyokodisha Rais, ilijitokeza bayana zaidi.

Kurasa zake kwenye mitandao ya kijamii vilevile hazikuangazia janga lililojitokeza, huku zikichapishwa tu shughuli zake Baku.

Walipaushuru walimimina kiasi kisichopungua Sh37 milioni kugharamia ndege ya kusafiri Baku, Azerbaijan.

Ndege hiyo aina ya Boeing 737-8DV (BBJ2) – itawagharimu walipaushuru hata zaidi wakati matumizi mengine ya kudumisha wajumbe wake yatajumuishwa.

Ndege hiyo ya kifahari iliyoundwa Septemba 2001, ni moja kati ya ndege za watu mashuhuri zinazomezewa mate zaidi ulimwenguni na inaweza ikawasafirisha angani wageni kati ya 19 na 50.

Kulingaan na Flight Radar, ndege hiyo ilisafiri kutoka Nairobi – Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Jomo Kenyatta – kuelekea Baku Mei 16, 2026 saa tatu na dakika kumi na nane usiku na kutua katika nchi hiyo ya Uropa Mei 17 saa kumi na moja na dakika tano alfajiri huku safari hiyo angani ikirekodiwa kuwa ya saa saba na dakika arobaine na saba.

Walipowasili, Rais na Mama Taifa Rachel Ruto walipokewa na Waziri wa Ulinzi Azerbaijan, Vuqar Mustafayev, na Balozi wa Azerbaijan, Kenya Sultan Hajiyev.

Ikikisiwa kuwa Rais atatumia ndege hiyo hiyo kurejea, gharama kwa mlipa ushuru itakuwa Sh37.14 milioni.

Taifa Leo haikupata kitambulisho cha mmiliki wa ndege hiyo ya kifahari wakati wa kuchapisha habari.

Hata hivyo, rekodi za ndege zinaashiria kwamba ndege aina ya Boeing 737-8DV (BBJ2) imesajiliwa kwa mmiliki wa kibinafsi San Marino.

Bado haijabainika ni nani atagharamia ukodishaji wa ndege hiyo ya kifahari, iwapo ni walipaushuru au rais mwenyewe, huku ikulu ikichelea kufichua maelezo ya kina kuhusu matumizi.

Umma haujasahau vilevile katika tukio sawia Mei 2024, Rais Ruto alipotumia ndege ya kifahari kusafiri Amerika, alijitetea, akisema alitumia Sh10 milioni kwa ziara yote na kuhifadhi mamilioni.

-TAFSIRI na Mary Wangari