Tathmini: Hapa kwa mafuta, ili kupunguza bei, serikali lazima isahau ushuru wa Sh74 kila lita
USHURU wa mafuta na faida za kampuni za uuzaji mafuta sasa zinatarajiwa kuangaziwa kwa makini huku serikali ikipambana na muda kupunguza bei ya mafuta ndani ya siku saba zijazo ili kuzuia mgomo mwingine wa sekta ya uchukuzi ambao unaweza kulemaza uchumi wa nchi.
Kutokana na bei ya mafuta duniani kuwa nje ya uwezo wa uthibiti wa serikali, pamoja na hazina ya ruzuku ya mafuta kukaribia kuisha, aina mbali mbali za ushuru unaotozwa bidhaa za petroli sasa umegeuka kuwa hoja kuu katika mazungumzo kati ya serikali na wahudumu wa magari ya uchukuzi.
Kenya ni miongoni mwa mataifa yenye ushuru mkubwa zaidi wa mafuta duniani.
Hivi sasa, lita moja ya petroli Nairobi inauzwa kwa Sh214.25 huku dizeli ikiuzwa kwa Sh232.86 baada ya kupunguzwa kwa Sh10.06 Jumatatu usiku.
Wizara ya Fedha hukusanya Sh74.05 na Sh67.83 kama ushuru kwa kila lita ya petroli na dizeli mtawalia.
Ushuru mkubwa zaidi ni wa matengenezo ya barabara wa Sh25 kwa kila lita, ukifuatiwa na VAT ya asilimia nane.
Waziri wa Usalama wa Ndani Kipchumba Murkomen alisema mazungumzo zaidi yataendelea katika wiki ijayo ili kupata suluhu ya kudumu.
Mwenyekiti wa Shirikisho la Sekta ya Uchukuzi wa Umma, Edwin Mukabane, alionya kuwa iwapo serikali haitachukua hatua ndani ya siku saba, mgomo huo utarejea.
Waziri wa Nishati Opiyo Wandayi alisema serikali tayari imetumia Sh13.9 bilioni kufadhili ruzuku ya mafuta katika miezi miwili iliyopita.
Serikali pia inatafuta njia za kudhibiti mfumuko wa bei uliopanda hadi asilimia 5.6 mwezi uliopita kutokana na kupanda kwa bei ya mafuta duniani kufuatia vita kati ya Amerika Israel na Iran.