Wafanyabiashara wasalia kuhesabu hasara ya mgomo
WAFANYABIASHARA kote nchini jana walikuwa wakikadiria hasara kubwa kufuatia maandamano ya Jumatatu yaliyogeuka kuwa vurugu katika miji kadhaa, ambapo makundi ya wahuni yalitumia fursa hiyo kuvamia biashara na kupora mali yakilalamikia kupanda kwa bei ya mafuta.
Ingawa maandamano hayo yalianza kwa amani, hali ilibadilika haraka na kuathiri shughuli za kiuchumi, kufungwa kwa biashara na kusambaratika kwa usafiri katika maeneo mbalimbali ya nchi.
Baadaye, washukiwa kadhaa walikamatwa na kufikishwa mahakamani Jumanne, huku wadau wa sekta ya uchukuzi wakitangaza kusitisha rasmi mgomo uliokuwa umeathiri usafiri.
Huko Nyeri, watu watatu walioshukiwa kuhusika na kufunga barabara wakati wa maandamano hayo ya kitaifa walifikishwa mahakamani na kuachiliwa kwa dhamana ya Sh50,000 kila mmoja au Sh20,000 pesa taslimu baada ya kukana mashtaka dhidi yao.
Mabw Paul Muchiri, Joseph Nderitu na Ibrahim Wachira, wameshtakiwa kwa kushiriki katika mkutano haramu kuzua vurugu katika barabara kuu mbili ndani ya Kaunti ya Nyeri.
Inadaiwa kuwa Mabw Muchiri na Nderitu walifunga barabara ya Nyeri–Nyahururu eneo la Nairutia, Kieni Magharibi, kwa kutumia mawe jambo lililozuia magari kupita kwa muda.
Bw Wachira anadaiwa kufunga barabara ya Karatina–Nyeri katika eneo la Ruring’u kwa kutumia tairi alizowasha moto, hali iliyosababisha msongamano mkubwa wa magari na usumbufu kwa wasafiri. Kesi hiyo itasikilizwa Juni 3.
Huko Murang’a, wafanyabiashara wadogo walieleza machungu yao baada ya vurugu hizo kuathiri moja kwa moja maisha yao ya kila siku.
Bi Beth Macharia, 34, anayeuza nafaka mjini Murang’a, alisema alipata hasara kubwa baada ya bidhaa zake kuvamiwa.
Wafanyabiashara wengine pia walikumbwa na janga hilo.
Bw Kamande Njogu (54) alipoteza bidhaa zake za mutura, supu na nyama ya ng’ombe zenye thamani ya Sh12,000 baada ya kuvamiwa na wahuni.
Wengine walilazimika kufunga biashara zao mapema kwa hofu ya usalama.
Hata viongozi wa eneo hawakuachwa salama, ambapo kituo cha burudani kinachomilikiwa na MCA wa eneo hilo, Machigo Karina, kilivamiwa na kuharibiwa huku bidhaa zikiporwa.
Huko Embu, kulikuwa na taharuki katika mji wa Kiritiri, Mbeere Kaskazini, baada ya waandamanaji kuvamia maghala ya serikali na kupora magunia ya mchele na maharagwe yaliyonuiwa familia zilizoathiriwa na njaa.
Mgomo huo pia ulisababisha upungufu mkubwa wa bidhaa muhimu katika Soko la Kongowea, Mombasa.
Kufuatia mgomo huo, wafanyabiashara sokoni walikuwa wakikadiria hasara huku upungufu mkubwa wa mboga, nafaka na bidhaa nyingine ukiripotiwa baada ya usafiri kuathirika.
Wasafirishaji wengi walikataa kupeleka bidhaa Mombasa kwa hofu ya mashambulizi au kuchomwa kwa malori yao.
Hali hiyo ilisababisha bei ya bidhaa kupanda huku bidhaa chache zilizokuwepo zikiuzwa kwa bei ya juu.
Mwenyekiti wa sehemu ya ndizi, Peter Mutisya, alisema kawaida hupokea malori sita hadi saba kwa siku lakini hakuna yaliyofika.
Malori yalirejea kwenye barabara kuu ya Mombasa–Nairobi jana, mgomo wa matatu ukiingia siku yake ya pili, hatua iliyowaletea afueni mamia ya abiria waliokuwa wamekwama njiani.
Hata hivyo, katika mji wa Wote, vijana walipambana na polisi kwa siku ya pili, wakiziba barabara kwa mawe na kuchoma matairi wakitaka bei ya mafuta ishuke kabla ya mgomo huo kufutwa jana mchana.
Wakati huo huo, polisi wanachunguza madai kwamba baadhi ya wahuni walioingia katika maandamano ya kulalamikia kupanda kwa bei ya mafuta mjini Kitengela Jumatatu waliletwa eneo hilo usiku wa kuamkia maandamano hayo kwa kutumia magari manne ya abiria yasiyo na alama maalum.
Maandamano hayo yaliyotarajiwa kuwa ya amani, yaligeuka vurugu baada ya makundi ya wahuni kuvamia mji wa Kitengela, kusababisha taharuki, kulemaza shughuli za usafiri na kuiba mali katika maduka mbalimbali.
Kamanda wa Polisi Kaunti ya Kajiado, Bw Alex Shikondi, alisema Jumanne kwamba watu 111 walikamatwa wakati wa vurugu zilizotikisa miji ya Kitengela, Ong’ata Rongai, Kiserian na Ngong.
Kati yao, washukiwa 74 walikamatwa Kajiado Kaskazini huku wengine 44 wakinaswa Kitengela. Wanatarajiwa kufikishwa kortini kwa makosa mbalimbali ikiwemo wizi.
Bw Shikondi alisema maafisa wa usalama walipokea taarifa za kijasusi kwamba baadhi ya waandamanaji waliletwa Kitengela mapema Jumatatu kwa magari ya abiria yasiyo na nambari za usajili.
“Tunaendelea kufuatilia taarifa kuwa magari manne ya uchukuzi wa umma yalionekana yakishusha watu karibu na Barabara ya Prison usiku wa Jumapili. Watu hao wanashukiwa kuchochea fujo na kuwahangaisha madereva pamoja na abiria,” alisema.