IEBC yataka Sh100 milioni kufadhili kampeni ya kusajili wapiga kura
TUME Huru ya Uchaguzi na Mipaka(IEBC), imeomba Bunge kuidhinisha Sh100 milioni kufadhili kampeni ya kuhamasisha raia kupitia vyombo vya habari kabla ya kuanza kusajili wapiga kura wapya 6.3 milioni 6.3 katika zoezi kubwa.
Tume hiyo, katika ombi lake la bajeti ya ziada kwa Kamati ya Haki na Masuala ya Kisheria ya Bunge la Kitaifa, imesema fedha hizo zitatumika katika zoezi la siku 30 la usajili wa wapiga kura litakaloanza Machi 30, 2026.
“Tume inapanga kuanza zoezi la Kuimarisha Usajili Endelevu wa Wapiga Kura kuanzia Machi 30, 2026 kwa muda wa siku 30, litakaloambatana na ushirikishaji mkubwa wa wadau na mahitaji zaidi ya vifaa na rasilimali kwa ajili ya utekelezaji wake,” IEBC iliambia kamati hiyo Jumatano.
Kwa mujibu wa tume hiyo, matarajio ya kusajili wapiga kura wapya 2.5 milionikatika siku 30 zijazo yanatokana na hali halisi ya idadi ya watu nchini, hasa vijana wengi ambao wamefikisha umri wa kupiga kura tangu zoezi la mwisho la usajili mkubwa lilipofanyika.
IEBC inalenga kuongeza wapiga kura wapya milioni 6.3 ili kufikia lengo la jumla la wapiga kura milioni 28.5 kabla ya uchaguzi mkuu wa 2027.
Kwa mujibu wa Kifungu cha 2 cha Sheria ya Uchaguzi, Sura ya 7, mchakato wa usajili wa wapiga kura unahusisha ukusanyaji wa taarifa binafsi pamoja na alama za mpiga kura kwa njia ya dijitali.
Tume hiyo inakabiliwa na changamoto kubwa ya kuwahamasisha wapiga kura wapya, hasa vijana ambao katika miaka ya nyuma wamekuwa wakipuuza zoezi hilo.
IEBC imewaambia wabunge kuwa kupitia kampeni kali za uhamasishaji na elimu kwa umma, ina matumaini ya kufikia malengo yake iwapo fedha zitapatikana.
Haya yanajiri huku takwimu za karibuni zikionyesha kuwa tume hiyo imesajili wapiga kura wapya 216,924 pekee katika kipindi cha miezi sita iliyopita.
Kwa mujibu wa takwimu hizo, kaunti zinazoongoza kwa idadi ya wapiga kura wapya ni Nairobi ikiwa na 40,388, ikifuatiwa na Kiambu (17,360), Mombasa ikiwa na 12,477, Kitui10,115 na Machakos ikiwa na 10,080.
Kaunti nyingine zilizosajili idadi kubwa ya wapiga kura wapya ni pamoja na Meru, Murang’a, Nakuru, Kakamega, Kisii na Bungoma.
Zoezi la Usajili Endelevu wa Wapiga Kura lilizinduliwa Septemba mwaka jana kwa mujibu wa wajibu wa kikatiba wa IEBC chini ya Ibara ya 88(4) ya Katiba.
Akizindua mpango huo, mwenyekiti wa IEBC Erastus Ethekon alisema zoezi hilo ni hatua muhimu ya kuhakikisha kila Mkenya anayestahili anapata nafasi ya kushiriki katika kuamua mustakabali wa nchi kupitia uchaguzi wa kidemokrasia.
“Zoezi hili linaelekezwa hasa kwa vijana waliotimiza umri wa miaka 18 na raia wote ambao bado hawajasajiliwa au wanaohitaji kubadilisha taarifa zao za kupiga kura,” alisema Bw Ethekon.