Afya na Jamii

Athari za kuvalisha mtoto viatu kabla hajaanza kutembea

Na WINNIE ONYANDO April 24th, 2026 Kusoma ni dakika: 4

MOJAWAPO ya maswali yanayozua mjadala katika malezi ya watoto wachanga ni kuhusiana na wakati ambapo mtoto anapaswa kuanza kuvalia viatu.

Kila mzazi haswa akina mama huvutiwa sana na hata kujawa na furaha wanapowaona watoto wao wachanga wakiwa wamevaa viatu mapema.

Baadhi huamua kuwanunulia wanao viatu wakiwa wachanga kwa sababu wao wenyewe walivaa viatu kwa mara ya kwanza wakiwa watu wazima.

Swala hili lilimvutia Daktari wa Watoto Varsha Hirani, kujaribu kuelewa misimamo na maoni ya wazazi tofauti.

Kupitia ukumbi wake kwenye mtandao wa kijamii wa WhatsApp wenye takriban wazazi 350, aliweka swali ili kukusanya maoni kuhusu suala la kuwavalisha watoto wachanga viatu.

Kulikuwa na majibu mseto. Karibu nusu waliamini watoto wanahitaji viatu mara tu wanapoanza kusimama huku wengine wakiamini viatu huwasaidia watoto kujifunza kutembea haraka.

Wengine wachache walidai kununua viatu vikubwa husaidia kuokoa pesa.

Lakini wataalamu wa afya ya watoto wanatahadharisha kuwa baadhi ya imani hizi ni potovu na zinaweza hata kuathiri ukuaji wa mtoto.

Kwa mujibu wa Dkt Varsha, viatu vinapaswa kuanza kutumika pale mtoto anapoanza kutembea kwa kujitegemea na kwa kujiamini hasa nje ya nyumba.

Hii ni kwa sababu kabla ya hatua hiyo, miguu ya mtoto bado inajifunza kubeba uzito wa mwili na kuzoea mazingira.

“Ndani ya nyumba, mtoto anaweza kubaki bila viatu au kuvaa soksi zisizoteleza ili kumkinga dhidi ya ajali,” anasema Dkt Varsha.

Anasema kuwa ni muhimu sana kutofautisha kati ya mtoto kuvaa viatu na kuhitaji viatu.

Watoto wachanga wanaweza kuvaa buti laini kwa ajili ya joto au mapambo lakini hawazihitaji kuwasaidia kujifunza kutembea.

“Viatu vinahitajika pale tu mtoto anapokutana na mazingira hatarishi kama vile ardhi yenye joto kali, baridi, uchafu au vitu vyenye ncha kali. Hapo ndipo viatu vinakuwa kinga si chombo cha kujifunza kutembea.”

Kwa upande mwingine, anasisitiza kuwa kutembea bila viatu kunafaa sana kwani husaidia katika ukuaji wa mtoto.

“Miguu ina maelfu ya mishipa ya fahamu ambayo hutuma taarifa kwa ubongo kuhusu mazingira. Hii huimarisha uwezo wa kusawazisha mwili, kuratibu harakati na kujenga ujasiri wa kutembea,” anaongeza.

Aidha, hisia za kugusa vitu mbalimbali kama sakafu baridi, nyasi au mchanga huchangia ukuaji wa ubongo.

Kulingana na ripoti ya National Library of Medicine, watoto wanaotembea miguu tupu hupata msisimko wa hisia unaoweza kuboresha uwezo wa kuzingatia, kutatua matatizo na hata kuimarisha uwezo wake wa kuzungumza.

Pia, kutembea bila viatu husaidia misuli midogo ya miguu kukua kwa kawaida na kusaidia kutengeneza umbo la mguu.

Anaonya kuwa kuvaa viatu mapema hasa vile vigumu au vizito kunaweza kuathiri namna mtoto anavyotembea.

“Viatu vigumu huathiri misuli ya miguu jambo linaloweza kusababisha udhaifu au hata miguu kuwa kombo.”

Vilevile, viatu vyenye soli nene au visigino vilivyoinuliwa vinaweza kubadilisha namna mtoto anavyokanyaga na kuongeza shinikizo kwenye vifundo vya miguu.

Kwa muda mrefu, hali hii inaweza kuathiri ukuaji wa kawaida wa mifupa ya miguu.

Ingawa kutembea bila viatu ni muhimu, daktari huyo wa watoto anasema kuwa si kila mazingira ni salama.

Ndani ya nyumba, anawashauri wazazi kutumia soksi zisizoteleza.

Nje ya nyumba, anawashauri wazazi kuchagua viatu vyenye sehemu ya mbele pana ili vidole vipate nafasi, soli laini na inayopinda kwa urahisi, visivyo na kisigino na vilivyotengenezwa kwa vifaa vinavyopitisha hewa kama pamba au ngozi laini.

Kwa watoto ambao bado hawajaanza kutembea, anasema ni sawa kuwavalisha buti laini za ngozi au soksi ili kulinda ngozi ya miguu.

Wazazi wanashauriwa kupima miguu yote miwili ya mtoto kabla ya kununua viatu na kuacha nafasi ya takriban sentimita moja na robo mbele ya kidole kirefu.

Ni muhimu pia mtoto awepo ili avijaribu viatu na kuhakikisha vinamfaa kabla ya kununua.

Hii ni kwa sababu utafiti uliochapishwa kwenye jarida la National Library of Medicine uliochambua maendeleo ya watoto wanaoanza kutembea, ilibainika kuwa kiatu kumtosha mtoto ni jambo muhimu zaidi kuliko aina ya kiatu.

Utafiti huo ulionyesha kuwa watoto wanaovaa viatu vinavyowiana vizuri na ukubwa wa miguu yao huonyesha maendeleo bora ya kutembea, ikiwa ni pamoja na uwezo wa kutembea kwa uthabiti.

Kipengele cha pili kilichoangaziwa ni kwamba viatu visivyotoshea vizuri viwe ni vikubwa kupita kiasi au vidogo vinaweza kuathiri namna mtoto anavyojifunza kutembea.

Kwenye utafiti huo, watoto waliovaa viatu visivyofaa walionekana kuwa na changamoto zaidi katika uthabiti wa hatua na uratibu wa mwili, jambo linaloweza kuathiri maendeleo ya harakati za msingi wanapokua.

Aidha, utafiti huo ulisisitiza kuwa katika hatua za mwanzo za ukuaji, mwili wa mtoto bado uko katika mchakato wa kujifunza na kuunda mifumo ya kawaida ya kutembea, hivyo shinikizo la nje kutoka kwa viatu visivyofaa linaweza kuingilia mchakato huu.

Hii ina maana kuwa mtoto anafaa kuvaa viatu vinavyofaa kiumri na kwa ukubwa ili kusaidia ukuaji wa kawaida wa miguu na mwendo.

Daktari Varsha pia anasema kuwa ni vyema kuchagua viatu vyenye soli laini na visivyoteleza na kuepuka viatu vilivyotumika maarufu kama mtumba.

Ukubwa wa viatu pia unapaswa kuangaliwa kila baada ya miezi miwili kwa sababu miguu ya mtoto hukua haraka.

Wazazi wengi huingiwa na hofu wanapoona miguu ya wanao haina umbo lakini hii ni hali ya kawaida kwa watoto wadogo.

Utafiti wa National Library of Medicine pia unaonyesha kuwa takriban asilimia 97 ya watoto walio chini ya miezi 18 huwa na miguu isiyo na umbo halisi kutokana na uwepo wa mafuta chini ya nyayo.

Kadri wanavyokua hali hii hupungua yenyewe na kufikia umri wa miaka 10 ni asilimia ndogo tu hubaki na hali hiyo.

Matibabu maalum au viatu vya kurekebisha mara nyingi havihitajiki isipokuwa pale mtoto anapopata maumivu makali au changamoto ya kutembea.

Kwa kifupi watoto hawahitaji viatu mapema kama wengi wanavyodhani bali wanahitaji uhuru wa kutumia miguu yao kujifunza kuhisi na kukua kwa kawaida.

Baadhi ya dhana potovu kuhusu viatu

Mtoto anahitaji viatu akianza kusimama ilhali ukweli ni kwamba viatu vinahitajika anapoanza kutembea nje.

Viatu husaidia mtoto kutembea haraka ilhali kutembea bila viatu humsaidia kujifunza kwa haraka zaidi kwa sababu anazoea mazingira na neva kutuma ujumbe kwa ubongo.

Watoto wanahitaji msaada wa umbo la mguu lakini ukweli ni kwamba umbo la mguu hujijenga kadri wanavyokua
Viatu vigumu hutoa uthabiti ilhali vinazuia ukuaji wa misuli.

Viatu vya juu hulinda kifundo cha mguu lakini nguvu ya kifundo hujengwa kupitia harakati za kawaida.

Kununua viatu vikubwa husaidia kuokoa pesa, hata hivyo ukweli ni kuwa viatu vikubwa ni hatari kwani mtoto anaweza kujikwaa na kuanguka.