Upinzani wapasuka Nigeria na kumpa Tinubu kazi mswaki 2027
ABUJA, Nigeria:
MATUMAINI ya Viongozi wa upinzani Nigeria kuungana na kumtoa kijasho Rais Bola Tinubu kwenye uchaguzi mkuu wa Januari mwaka ujao yanaendelea kudidimia.
Hii ni baada ya vinara wakuu Peter Obi na Rabiu Kwankwaso kujiondoa kwenye muungano mkubwa wa upinzani na kuunda muungano wao wa kisiasa. Wamechukua hatua hiyo kutokana na uhasama wa ndani kwa ndani ambao umekuwa katika upinzani kwa muda sasa.
Obi na Kwankwaso walimaliza wa tatu na nafasi ya nne mtawalia kwenye uchaguzi wa urais mnamo 2023.
Awali wawili hao walikuwa wameungana na Kiongozi Mkuu wa upinzani na makamu wa rais wa zamani Atiku Abubakar pamoja na wanasiasa wengine wenye ushawishi mkubwa chini ya Muungano wa Muungano wa African Democratic Congress (ADC).
Muungano huo ulikuwa mkubwa na ulikuwa ukipigiwa upato kutwaa mamlaka mwaka ujao. Mnamo Aprili 25 vinara wa ADC walikubali kumuunga mkono mwaniaji mmoja wa urais mwakani.
Obi anayetoka kusini mwa Nigeria aliwasisimua wapigakura wachanga mnamo 2023 na kuvutia umati mkuwa. Alitangaza mnamo Jumatatu kuwa hayuko tena ADC.
Kiongozi huyo alifichua kuwa alichukua hatua hiyo kutokana na uhasama wa ndani kwa ndani, kesi za korti zisizokamilika, kutiana shaka na mgawanyiko usiokuwa na kikomo.
Kwankwaso, mwenye ushawishi kutoka kaskazini mwa Nigeria pia aliondoka na kuungana na Obi kwenye muungano mpya wa Nigeria Democratic Congress (NDC).
“Kutokana na matukio haya na hali ambayo tumejipata, itabidi tutathmini upya nia ya upinzani kuwa na mgombeaji mmoja wa kisiasa,” akasema Msemaji wa ADC Bolaji Abdullahi.
Kuondoka kwa wanasiasa hao kunaonekana kuwa nafuu kwa Rais Tinubu ambaye alishinda uchaguzi mkuu uliopita kwa asilimia 35 za kura zilizopigwa.
Viongozi wote wa upinzani walikuwa na jumla ya asilimia 60 ya kura na ADC ilikuwa inataka kuzuia kupoteza huko kwa kuungana 2027.
“Uhalisia ushaanza kuonekana na tamaa zao zipo wazi. Hawaendi mahali wakiendelea kugawanyika hivi,” akasema Mchanganuzi wa kisiasa Cheta Nwanze kutoka Lagos.
Ushindani kati ya Atiku ambaye amekuwa akiwania kutoka kaskazini na Obi ambaye amechipuka na anatoka eneo hilo pia, kumetajwa kama kiini cha mpasuko huo.
Msemaji wa Afisi ya Rais Bayo Onanuga alimkashifu Obi kwa kujiondoa kwenye muungano wa kisiasa akisema ni kiguu na njia na mwanasiasa mbinafsi.
“Hawezi kupigania tikiti ya ADC na Atiku au Amaechi na anapenda tu njia iliyoonyoka ambayo itampeleka tu kupoteza jinsi ilivyokuwa 2023,” akaandika Bayo kwenye X.
Alikuwa akiwarejelea Abubakar na Waziri wa zamani wa uchukuzi Rotimi Amaechi ambaye pia ni mmoja wa vinara wa upinzani.
Rais aliye mamlakani amepoteza tu mara moja Nigeria na hiyo ni 2015 pale ambapo Goodluck Jonathan alikiri kushindwa na marehemu Muhammadu Buhari baada ya upinzani kuungana.