Kimataifa

Waasi wa Houthi wanaoungwa mkono na Iran walemea Saudi Arabia kwa makombora

Na REUTERS September 16th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

RIYADH, Saudi Arabia

WAASI wa Houthi wanaoungwa mkono na Iran wameanzisha wimbi jipya la mashambulizi dhidi ya Saudi Arabia, hatua ambayo imeongeza wasiwasi kuhusu usalama wa usafirishaji wa mafuta katika Mashariki ya Kati.

Serikali ya Yemen ilisema kuwa Wahouthi wapo pwani ya magharibi ya Yemen, kando ya Bahari ya Shamu ambapo wamenogesha mikakati ya kushambulia Saudi Arabia.

Wahouthi wenyewe walisema walirusha makombora kadhaa na ndege zisizo na rubani katika kituo cha kijeshi cha Khamis Mushait kusini mwa Saudi Arabia.

Walisema walilenga ndege, uwanja wa ndege na maghala ya risasi, kulipiza kisasi mashambulizi ya anga ya Saudi Arabia nchini Yemen.

Serikali ya Saudi Arabia imetoa tahadhari kwa wanaopanga kuzuru miji minne ya kusini. Saudi Arabia ilisema raia 13 walijeruhiwa katika mashambulizi hayo ya Wahouthi.

Mashambulizi hayo yameongeza shinikizo kwa usafirishaji wa mafuta wa Saudi Arabia baada ya shambulizi la anga Alhamisi kusababisha bomba la mafuta linalounganisha mashariki na magharibi mwa nchi hiyo kusitisha shughuli.

Saudia ililaumu wanamgambo hao wanaoungwa mkono na Iran kutokana na shambulizi hilo.

Wafanyabiashara wa mafuta walisema kufungwa kwa muda mrefu kwa bomba hilo kunaweza kuathiri hadi asilimia nne ya usambazaji wa mafuta duniani, hasa wakati Mkondo wa kupitisha mafuta wa Hormuz ukiwa bado umefungwa na Iran.

Wakati huo huo, matumaini ya diplomasia yalipungua baada ya nchi za Ghuba kuahirisha mazungumzo yaliyopangwa na Iran kuhusu kufunguliwa tena kwa Mlango wa Hormuz.

Kabla ya vita kati ya Amerika-Israel dhidi ya Iran, Strait of Hormuz ilikuwa ikipitisha asilimia 20 ya mafuta yanayouzwa duniani.

Oman, iliyokuwa imepanga kuandaa mkutano huo, ilitangaza kuwa umeahirishwa.

Iran ilisema Saudi Arabia ndiyo iliyoomba kuahirishwa.

Rais wa Amerika Donald Trump alisema Iran ilikuwa tayari kufanya makubaliano, lakini Mohsen Rezaei, katibu wa Baraza Kuu la Usalama wa Taifa la Iran, alikataa kauli hiyo na kusema hakuna mazungumzo hadi masharti ya Iran yatimizwe.

Saudi Arabia imekuwa ikiongoza vita dhidi ya Wahouthi tangu 2015. Ingawa mapigano yalipungua baada ya pande zote kuafikia makubaliano ya kusitisha mapigano, vita vilianza tena mwezi huu.

Kuendelea kwa mapigano na tishio kwa Mlango wa Hormuz kunazua hofu zaidi kwamba usambazaji wa mafuta duniani unaweza kuvurugika, hali ambayo huenda ikaendelea kuweka shinikizo la kupanda kwa bei ya mafuta.