Jamvi La Siasa

Ukaribu wa Ababu na chama cha ODM waibua joto la kisiasa

Na CECIL ODONGO April 19th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

UHUSIANO wa karibu unaochipuka chini kwa chini baina ya aliyekuwa Mbunge wa Budalang’i Ababu Namwamba na ODM, umeibua maswali iwapo waziri huyo wa zamani huenda analenga kuwania kiti cha kisiasa baada ya kuwa kwenye baridi tangu 2017.
Jumanne wiki jana mbunge huyo wa zamani aliyekuwa na mikuki mikali ya kisiasa, alitundika picha mtandaoni akiwa na kinara wa ODM, Dkt Oburu Oginga.
Picha hiyo akiwa amemshika Dkt Oginga mkono wakitabasamu ilizua maswali zaidi iwapo Namwamba anapanga kurejea katika chama hicho cha chungwa.
“Ningependa kumtakia Dkt Oginga kila la heri anapoongoza chama kipindi hiki muhimu cha mpito. Vyama imara hujenga demokrasia thabiti,” akaandika.
Namwamba aliweka picha hiyo siku chache baada ya kuhudhuria Kongamano Maalum la Wajumbe (SDC) wa ODM ambapo alizungumzia wakati wake akiwa katibu mkuu wa chama hicho kati ya 2014-2016 alipotwaa nafasi hiyo kutoka kwa Profesa Anyang’ Nyong’o.
“Ningependa kumshukuru mwenyekiti wetu na pia kiongozi wa chama. Hapa nawaona wale tulikuwa nao pamoja chamani. Tumetoka mbali, na nakumbuka mwaka 2008 niliapa kuwa mtiifu na mwaminifu kwa ‘Rais’ Raila Odinga,” akaeleza Namwamba.
Alikuwa akirejelea uchaguzi tata wa 2007 ambapo akiwa mbunge kwa mara ya kwanza, aliamua kula kiapo kuonyesha uaminifu wake kwa Odinga badala ya Rais Mwai Kibaki.
“Naomba tusonge mbele na tuchukue mamlaka na ninawahakikishia kwamba tutaendelea kuwa pamoja. Safari ambayo tulianza miaka 20 iliyopita ya kusaka mamlaka lazima iendelee hata tunapoombea roho ya Odinga,” akasema.
Masaibu ya Namwamba ndani ya ODM yalianza wakati wa uchaguzi uliovurugika wa chama mnamo 2014, aliposhutumiwa na baadhi ya viongozi kuwa msaliti.
Wakati huo alikabiliwa na madai kwamba alikuwa akishirikiana na utawala wa Uhuru Kenyatta na William Ruto ili kudhoofisha ODM.
Hata hivyo, alikana madai ya usaliti akisema ushirikiano wake ulikuwa kwa ajili ya kuleta maendeleo kwa wakazi wa Budalang’i na kanda ya Magharibi.
Kwa sasa Namwamba anahudumu kama Balozi Mkuu wa Kenya nchini Uganda, baada ya kuteuliwa na Rais William Ruto.
Awali alikuwa Mwakilishi wa Kudumu wa Kenya katika Afisi ya Umoja wa Mataifa (UN) jijini Nairobi pamoja na Shirika la Mazingira la Umoja wa Mataifa (UNEP).
Namwamba alihudumu kama mbunge wa Budalang’i kati ya 2007 na 2017, akifahamika kama mtetezi mkubwa wa Odinga na ODM.
Alipoteza kiti hicho kwa Raphael Wanjala uchaguzi wa 2017.
Kabla uchaguzi mkuu wa 2022 alijiuzulu wadhifa wake kama naibu waziri akajiunga na chama cha UDA chake Rais Ruto, ingawa hakugombea kiti chochote huku akishiriki tu kampeni za urais.
Baada ya serikali ya sasa kuingia madarakani aliteuliwa Waziri wa Michezo na Masuala ya Vijana.
Hata hivyo, alikuwa miongoni mwa mawaziri waliotemwa baada ya kuvunjwa kwa Baraza la Mawaziri mnamo Julai 2024 kutokana na maandamano ya kupinga Mswada wa Fedha wa 2024.
Ukuruba wake na ODM unajiri wakati chama hicho kimegawanyika katika makundi mawili: Linda Ground inayoongozwa na Dkt Oginga, na Linda Mwananchi chini ya Katibu Mkuu wa ODM na Seneta Wa Nairobi, Edwin Sifuna.
Akitoka Kaunti ya Busia, ambapo ODM ilishinda viti vitano kati ya saba vya ubunge pamoja na ugavana na uwakilishi wa wanawake, wachanganuzi wanasema huenda Namwamba analenga kiti 2027 kupitia ODM.
Kwa mujibu wa mchanganuzi wa masuala ya kisiasa Martin Andati, Bw Namwamba ni mwanasiasa mchapakazi ambaye amefanya vyema katika utumishi wa umma.
“Kutokana na yale yanayoendelea kuna wale ambao wanamtaka Namwamba arejee ODM na hata awe katibu mkuu. Shida ni kuwa akikubali kuchukua nafasi ya Sifuna atakuwa akionekana kama msaliti,” aeleza