JAMVI LA SIASA: Uwakilishi ‘hewa’ wa vijana kaa moto kwa Linda Ground
KINARA wa ODM Dkt Oburu Oginga amekuwa akijirejelea kama ‘kiongozi wa vijana’ kudhihirisha kuwa uongozi wake unamakinikia masuala ya vijana na changamoto zinazowakumba.
Licha ya umri wake mkubwa wa miaka 82 seneta huyo wa Siaya alianza kujihusisha na Gen Z mnamo 2024 baada ya vijana kuandaa maandamano dhidi ya serikali ya kupinga Mswada wa Fedha 2024.
Licha ya Dkt Oginga kuendelea kujihusisha na vijana uhasama mkubwa unaendelea kutokota ndani ya Linda Ground anayoingoza kuhusu uwakilishi wa vijana.
Mnamo Jumatano, Seneta wa Migori Eddy Oketch alilipuka na kudai kuwa wazee ndio sasa wanaendesha Linda Ground huku vijana wakitengwa.
Oketch anayehudumu muhula wake wa kwanza alikasirishwa na bango la vuguvugu la vijana ODM kuhusu mkutano ambao unaandaliwa Malindi leo.
Bango hilo la ODM Youth League lilikuwa na picha za Dkt Oginga, magavana Gladys Wanga (Homa Bay), Simba Arati (Kisii), Gideon Mung’aro (Kilifi), Kiongozi wa Wachache Bungeni Junet Mohamed na Waziri wa Madini Hassan Joho.
“Hapa ndiyo shida huanzia chamani, vijana hawahusishwi kwenye uongozi na mikutano hii,” akasema seneta huyo.
“Kwa mwaka moja sasa nimejaribu kuzungumzia suala hili na ngazi mbalimbali za chama. Pia masuala ya vijana na uongozi wa chama lakini hakuna kinachofanyika,” akaongeza Oketch anayehudumu muhula wake wa kwanza.
Alizua maswali kwa nini picha za viongozi vijana kama Mbunge wa EALA Winnie Odinga, Mbunge maalum Umulkher Harun Mohamed (Umi), Hezena Lematin (Seneta maalum), Mbunge wa Lang’ata Felix Odiwuor au Mbunge wa Malindi Amina Mnyazi hazikuwa kwenye bango hilo.
Kabla ya Oketch kupiga kelele kuhusu suala hilo, Diwani wa Kileleshwa Robert Alai alikuwa amemvamia Rais wa vuguvugu la vijana wa ODM (ODM Youth League) John Ketorah akimtaka ajiuzulu kwenye wadhifa wake.
Alai alidai kuwa Ketorah, ambaye anahudumu muhula wake wa pili, si kijana na anastahili kuondoka.
“Utatakaje UDA ikuheshimu kama hauheshimu katiba yako. Mtu mwenye umri wa miaka 41 bado anaendelea kuwa Rais wa Vijana wa ODM,” akaandika Alai kwenye kurasa zake za mitandao ya kijamii wiki jana akimlenga Ketorah.
ODM ilipoandaa kongamano lake la vijana Jumapili iliyopita Nairobi, Alai alisema hafla hiyo haikuwa na maana iwapo Ketorah atasalia kuwa mamlakani.
“Chama lazima kimwondoe Ketorah kama kiongozi wa vijana na wawe na kiongozi kijana achukue nafasi yake huku chama kikikumbatia mbinu ya kujivumisha,” akaongeza Alai.
Kwenye mahojiano na Jamvi, Ketorah alikiri kuwa vijana walionekana kutengwa kwenye kongamano lao la Nairobi wikendi iliyopita.
Alisema viongozi wa kitaifa walichukua usukani kutokana na hofu kuwa hafla hiyo ingeingiliwa na kutekwa na vijana kutoka kundi pinzani la Linda Mwananchi.
“Hilo lilifanyika kwa sababu hawakutaka vijana kutoka mrengo pinzani kuingilia hafla hiyo. Mtaanza kuona vijana kwenye makongamano yanayokuja,” akahoji.
ODM imepanga kuandaa misururu ya makongamano ya vijana kwenye kaunti 40 na watakuwa Kwale na Taita Taveta mnamo Mei 9 na Mei 10 mtawalia.
Kuhusu Oketch, rais huyo wa vijana alimrejelea kama kiongozi asiye na shukrani ambaye sasa anatumika kupiga vita vijana ambao ndio walimpa wadhifa wake.
“Ni mtu mbinafsi. Ni mimi nilimpendekeza kutoka akademia yetu ya wawaniaji chipukizi na kushawishi chama kimpe tikiti ya kuwania useneta. Yeye ni seneta kwa sababu ya vuguvugu hili letu la vijana ambalo analidharau sasa,” aliongeza Ketorah ambaye analenga ubunge cha Kajiado Mashariki kupitia ODM mnamo 2027.
Rais huyo wa vijana hata alidai kuwa bango ambalo lilisababisha Bw Oketch kupiga kelele halikutoka kwa ODM.
Kuhusu Bw Alai, rais huyo alikiri kuwa umri wake upo juu lakini akasema alipochukua usukani, alikuwa bado kwenye tapo la umri unaohitajika.
“Nahudumu muhula wangu wa pili na wa mwisho kwa mujibu wa katiba yetu. Mbona anataka nijiuzulu na kuondoka katikati ya muhula wangu? Yeye si mwanachama wa vuguvugu letu na pia si afisa wa chama, kwa hivyo aachane na umri wangu,” akasema.
Bw Ketorah alichukua uongozi wa ODM Youth League mnamo 2014 baada ya aliyekuwa mshikilizi wa wadhifa huo Waziri wa zamani wa Michezo Rashid Mohamed kuondoka na kujiunga na mrengo wa UhuRuto kuelekea uchaguzi mkuu wa 2017.
“Rashid alipoondoka, vuguvugu hili nusura life lakini tumelijenga na sasa ni imara. Hatutayumbishwa na wivu kwa sababu wale wanaofanyia kazi maadui wetu sasa wanamakinikia chochote kile kuvuruga chama,” akasema.
Mbunge wa Makadara George Aladwa amekuwa kati ya viongozi ambao wanapigania uwakilishi wa vijana kwenye ngazi ya juu ya chama.
Bw Aladwa amekuwa akishinikiza kuwa Bi Winnie ambaye sasa ni mwakilishi wa ODM Nairobi, nafasi iliyokuwa ikishikiliwa na babake Raila Odinga, awe mmoja wa manaibu viongozi wa chama.
Wakati ambapo Linda Ground inapambana na suala la vijana kwenye uongozi wao, kundi pinzani la Linda Mwananchi nalo limewakumbatia.
Linda Mwananchi ina mchanganyiko wa viongozi wakongwe kama Gavana wa Siaya James Orengo na viongozi vijana kama Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino, mwenzake wa Saboti Caleb Amisi, Oundo Mudenyo wa Funyula na hata Katibu wa ODM Edwin Sifuna.