Habari

Oparanya awaonya viongozi wa ODM dhidi ya kupuuza eneo la Magharibi

Na DAVID MUTHOKA April 26th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

WAZIRI wa Vyama vya Ushirika na Maendeleo ya Biashara Ndogo na za Kati, Wycliffe Oparanya, ameonya kundi la Linda Ground ndani ya chama cha Orange Democratic Movement (ODM)linaloongozwa na Oburu Oginga, akisema eneo la Magharibi linaweza kukitema iwapo litaendelea kupuuzwa.

Akizungumza akiwa Lugari wakati wa hafla ya kutoa hundi za hazina ya Uwezo, Hazina ya Biashara ya Wanawake na Hazina ya Maendeleo ya Biashara ya Vijana, Bw Oparanya alisema viongozi wa sasa wa ODM wanapaswa kuheshimu eneo hilo kama ilivyokuwa wakati wa marehemu Raila Odinga.

Alisema kuwa kuna dalili za kuongezeka kwa mvutano ndani ya chama hicho, akilaumu kundi la Oburu kwa kudharau mchango wa eneo la Magharibi katika siasa za ODM.

“Tunataka tuwaambie wale viongozi wa ODM, safari hii wasituchukulie kwa mzaha.”

Raila alikuwa anatuheshimu, na wale waliopo sasa lazima watupe heshima. Wasipofanya hivyo, tutawaambia kwaheri,” alisema Oparanya.

Aidha, alieleza kuwa viongozi wa Magharibi walikuwa mstari wa mbele katika chama hicho enzi za Raila, lakini sasa wanahisi kutengwa huku maamuzi muhimu yakifanywa bila kuhusisha eneo hilo.

“Sisi tulikuwa karibu na Raila, tulikuwa viongozi katika chama. Sasa wanaendelea tu na mambo yao bila hata kujua sisi kama Magharibi tunataka mwelekeo huo,” aliongeza.

Kauli hiyo inaashiria mgawanyiko unaozidi kujitokeza ndani ya ODM huku makundi tofauti yakianza kuvutana kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027.