Trump atuma wajumbe Pakistan, Iran ikiendelea kukaa ngumu
WAJUMBE wa Amerika, Steve Witkoff na Jared Kushner, walisafiri Jumamosi kuelekea Pakistan kwa mazungumzo ya amani na Iran.
Kulingana na msemaji wa White House, Karoline Leavitt, Wairan walitaka mazungumzo.
Pia, aliongeza kuwa Makamu wa Rais wa Amerika, JD Vance, alikuwa tayari kusafiri ikiwa mazungumzo hayo yangeonyesha mafanikio.
Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran, Esmail Baqaei, alisema yeye na Waziri wa Mambo ya Nje, Abbas Araghchi, waliwasili mjini Islamabad Ijumaa jioni, na kwamba Araghchi angekutana na maafisa wa ngazi za juu wa Pakistan, akikanusha kuwepo kwa mazungumzo na Amerika.
“Hakuna mkutano uliopangwa kufanyika kati ya Iran na Amerika. Maoni ya Iran yatawasilishwa kwa Pakistan,” alikanusha Baqaei.
Kabla ya kauli ya Baqaei, Waziri wa Ulinzi wa Amerika, Pete Hegseth, alisema Tehran ina nafasi ya kufikia makubaliano mazuri, akisisitiza kuwa wanachotakiwa kufanya ni kuepuka silaha za nyuklia kwa njia inayoweza kuthibitishwa.
Katika mkutano na wanahabari Ijumaa, Hegseth pia alionya kuwa mzozo unaohusisha Hormuz, ulitatiza usafirishaji wa mafuta na kuongeza athari kote duniani.
Amerika na Israeli zilianza mashambulizi dhidi ya Iran Februari 28, na baadaye Tehran ikaweka vikwazo kwa usafirishaji kupitia Mkondo wa Hormuz.
Hatua hizi zimepelekea bei za mafuta kupanda kwa kasi duniani kote.
Akizungumza na waandishi wa habari Ijumaa, Leavitt alisema Trump aliamua kuwatuma Witkoff na Kushner Islamabad ili kuwasikiliza Wairan.
Aliongeza kuwa Rais wa Amerika yuko tayari kila wakati kuipa diplomasia nafasi.
“Tumeshuhudia maendeleo fulani kutoka upande wa Iran katika siku chache zilizopita,” alisema Leavitt.
Wakati huo huo, ubalozi wa Iran mjini Islamabad ulisema Araghchi alipanga kufanya mazumgumzo na kujadili maendeleo ya kikanda.
Wiki jana, Trump na Hegseth walisisitiza kuwa Amerika haisukumwi na shinikizo la kumaliza vita na Iran.
Hata hivyo, habari kwamba mazungumzo kati ya Amerika na Iran yanaendelea mwishoni mwa wiki hii yalioonyesha wazi tofauti kati ya kauli za umma za utawala huo na juhudi za siri za White House za kutafuta njia ya kumaliza vita.
Hali hii inaashiria kuwa pande zote mbili zinatafuta suluhu, licha ya jumbe zinazokinzana kutoka kwa Trump na msimamo mkali wa Tehran.
JD Vance aliongoza wajumbe wa Amerika katika mkutano wa kwanza wa mazungumzo mapema mwezi huu lakini hadi sasa hajathibitishwa kushiriki mazungumzo ya wikendi hii.
Iwapo Vance hatahudhuria, huenda ikawa ishara kuwa hakutakuwepo na mafanikio makubwa.
Japo, kuendelea kwa mazungumzo kunaonyesha kuwa Amerika na Iran zina nia ya kufikia makubaliano, Tehran kuendelea kukaa ngumu kutaashiria kuwa juhudi zote za kujaribu kutafuta suluhu la kudumu zitakuwa zimeambulia patupu.