Serikali ya Sakaja kufuliza Sh1.7B kila mwezi kulipa mishahara
MADIWANI wa Bunge la Kaunti ya Nairobi wameidhinisha mpango wa serikali ya kaunti kukopa hadi Sh1.7 bilioni kila mwezi kutoka Sidian Bank ili kusaidia kulipa mishahara ya zaidi ya wafanyakazi 19,000 wa kaunti kwa wakati.
Mpango huo unatokana na makubaliano (MOU) kati ya Serikali ya Kaunti ya Nairobi na benki hiyo, na unalenga kuziba pengo la kifedha mgao wa fedha kutoka serikali kuu unapochelewa au mapato ya ndani kupungua.
Mwenyekiti wa Kamati ya Bajeti na Fedha ya Bunge la Kaunti, Wilfred Odalo, alisema kamati hiyo ilipitia makubaliano hayo kabla ya kuyaidhinisha ili kuhakikisha wafanyakazi wanalipwa kwa wakati na huduma kwa wakazi haziathiriki.
Kwa mujibu wa makubaliano hayo, Sidian Bank itatoa huduma za kusaidia ulipaji wa mishahara na kuruhusu kaunti kupata mkopo wa hadi Sh1.7 bilioni kila mwezi.
Hata hivyo, benki itatoza ada ya asilimia 0.5 ikiwa deni halitalipwa ndani ya siku 60.
Kiongozi wa wachache katika bunge hilo, Anthony Kiragu, alisema mpango huo utawezesha shughuli za kaunti kuendelea bila kukwama kutokana na ucheleweshaji wa mishahara.
Maafisa wa kaunti walisema walichagua Sidian Bank baada ya benki nyingine mbili kujiondoa kutokana na ada zao kuwa juu zaidi.