Viongozi wamtetea Katibu wa UDA Omar
VIONGOZI mbalimbali wa kisiasa na kijamii wamejitokeza kumtetea Katibu Mkuu wa UDA, Hassan Omar, kufuatia wito wa baadhi ya watu kutaka ajiuzulu kutoka wadhifa wake.
Akizungumza katika mkutano na wanahabari, Bw Said Twaha alisema kuwa kauli ya Bw Omar kuhusu ardhi ilitafsiriwa vibaya.
Alieleza kwamba Katibu huyo hakumaanisha kuchukua ardhi ya watu, bali alisisitiza kuwa ardhi iliyonyakuliwa isivyo halali inapaswa kurejeshwa kwa wamiliki wake wa awali .
“Sisi tuko nyuma ya Bw Sarai, na wanataka ajiuzulu ni wakabila wanataka kuchukua nafasi hiyo iliyotengewa watu wa Pwani,” alisema Bw Twaha.
Kwa upande wake, kiongozi wa vijana Suleiman Hassan alisema hakuna sababu ya Bw Omar kujiuzulu. Alibainisha kuwa nafasi mbalimbali ndani ya chama zilitolewa kwa kuzingatia uwiano wa kikanda ili kuhakikisha kila eneo la nchi linawakilishwa ipasavyo.
Naye Mohammed Jere, ambaye ni kiongozi katika jamii ya Wasomali, alisisitiza kuwa Hassan Omar amekuwa kiungo muhimu katika chama hicho.
Alionya kuwa kuondolewa kwake kunaweza kusababisha baadhi ya wanachama kutoka jamii ya Wasomali kukipuuza au hata kukihama chama cha UDA.
“Viongozi hao pia wanaotaka Bw Omar aondolewe madarakani, wakisema kuwa hoja zao zinaegemea ukabila badala ya masuala ya utendaji kazi. Si vyema kutumia tofauti za kikabila kama msingi wa kufanya maamuzi ya kisiasa,” alisema Bw Jere.
Kwa upande wake, Francis Maina alisema Kenya inapaswa kuendelea kuimarisha umoja wa kitaifa na kuepuka siasa za ukabila.
Alisisitiza kuwa viongozi wanapaswa kuhukumiwa kwa misingi ya utendaji wao na si kwa asili au jamii wanayotoka.
Viongozi hao walitoa wito kwa wanachama wa UDA kuendelea kumuunga mkono Bw Omar na kudumisha mshikamano ndani ya chama.