Wanafunzi Baringo wahatarisha maisha yao huku wakikabiliana na Viboko, Mamba wakienda shule
SAA moja unusu asubuhi, watoto walijikusanya kimya kimya kando ya ufuo wa Ziwa Baringo, karibu na mahali ambapo barabara ya lami ilikuwa ikipita zamani.
Leo, barabara ya Loruk-Chemolingot imefunikwa kabisa na maji kutokana na mafuriko.
Wakishika mikoba yao ya shule huku baadhi wakitetemeka kutokana na upepo wa ziwa, wanafunzi wa Shule ya Msingi ya Loruk walisubiri kwa wasiwasi boti ndogo ya mbao ambayo ndiyo njia pekee ya kuwafikisha shuleni, umbali wa takriban mita 500 tu.
Karibu nao, makundi ya viboko yalikuwa majini mita chache tu milio yao mikali ikisikika kote kandokando ya eneo lililofurika.
Mara kwa mara, mamba pia hujitokeza kabla ya kutoweka tena chini ya maji, lakini kwa watoto hao, safari hii ya kutisha imekuwa sehemu ya maisha yao ya kila siku.
Kwa wanafunzi kutoka vijiji vya Cherelyo, Kakipich, Parichar na Kiplechony, safari ya kwenda shule imekuwa kamari ya kila siku dhidi ya kifo baada ya kupanda kwa maji ya Ziwa Baringo na kufunika barabara ya Loruk-Chemolingot.
Kilichokuwa matembezi mafupi ya mita 500 sasa kimegeuka kuwa changamoto kubwa na hatari, huku zaidi ya wanafunzi 200 wakitegemea boti moja kuvuka kila siku.
Boti hiyo hubeba watu wanane kwa safari moja, lakini imelemewa na mahitaji, ikiwavusha watoto kwa zamu bila mpangilio, bila jezi za kuokoa maisha na bila wahudumu wa usalama.
Kila mtoto hulipa Sh20 kwa safari moja, na kwa wanaorudi nyumbani mchana na kurudi tena shuleni, gharama huweza kufikia Sh80 kwa siku, mzigo mkubwa kwa familia maskini.
Njia mbadala ipo, lakini ni mwendo wa kilomita tano kupitia eneo lenye mafuriko, safari ndefu na ngumu kwa watoto wadogo.
Hali ya shule yenyewe pia ni ya kusikitisha kwani baada ya kushuka kutoka boti, wanafunzi hulazimika kupita kwenye maji yaliyofunika sehemu ya eneo la shule kabla ya kufika darasani.
Sehemu kubwa ya shule imezama, ikiwa ni pamoja na viwanja vya michezo, madarasa matano, vyoo vinane na bweni ya wavulana iliyokuwa ikihifadhi zaidi ya wanafunzi 60.
Vichaka vinavyozidi kuota vimegeuza eneo la shule kuwa hatari, huku hofu ya nyoka ikizidi kutokana na mazingira.
Kwa kuwa hakuna ua, viboko na mamba sasa huingia ndani ya eneo la shule, na kuhatarisha maisha ya wanafunzi na walimu.
Shuleni, wanafunzi hutumia ngazi ya mbao ya muda kupita maeneo yaliyofurika.
Wanafunzi wanaolala kwenye bweni pia wameathirika, ambapo wavulana wamehama kutoka bweni lililozama na sasa hulala kwenye darasa la chekechea ambalo hutumika pia kama darasa mchana.
Tatizo la mafuriko katika shule hiyo lina historia ya muda mrefu tangu 2006, wakati darasa la chekechea lilipozama na kulazimika kuhamishwa.
Mwaka 2020, mafuriko mengine yaliathiri bweni, vyoo na uwanja wa michezo, huku barabara pia zikifutika.
Serikali ilipanga kuhamisha shule hiyo kwenda eneo salama la Cherelyo, baada ya wananchi kuchangia zaidi ya ekari 50 za ardhi.
Kamishna wa Kaunti ya Baringo Stephen Kutwa alisema serikali inaendelea kutathmini shule zilizoathirika zaidi ili kuzipa kipaumbele cha uhamisho.
Alisema mipango ipo ya kuhamisha shule hiyo wiki ijayo, hata kwa kuweka mahema ya muda miundombinu ya kudumu ikijengwa.