Siasa

Ida: Siwezani na siasa, acha Winnie, Oburu watambe

Na BENSON MATHEKA April 19th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

MJANE wa aliyekuwa Waziri Mkuu Raila Odinga, Ida Odinga, amepuuzilia mbali wito wa kuingia katika siasa kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027, akisisitiza kuwa hana nia ya kuwania wadhifa wowote wa kisiasa nchini.

Akizungumza Jumatatu wiki hii, Ida alieleza kuwa ukimya wake wa muda mrefu haukuwa ishara ya kupanga mikakati ya kisiasa, bali ulitokana na kipindi cha maombolezo kufuatia kifo cha mumewe.

“Nilipompoteza mume wangu, nilikuwa katika kipindi cha maombolezo ambacho kilikuwa muhimu sana kwangu. Sikuweza kushiriki masuala yoyote ya kisiasa wakati huo,” alisema.

Ida, ambaye pia ni Balozi wa Kenya katika Shirika la Mazingira la Umoja wa Mataifa (UNEP), alisisitiza kuwa siasa si eneo lake, akijitambulisha kama mfanyabiashara na mwanadiplomasia.

“Binafsi mimi si mwanasiasa. Marehemu mume wangu alikuwa mwanasiasa, binti yangu pia yuko katika siasa, na shemeji yangu pia. Lakini mimi nimechagua njia tofauti,” aliongeza.

Alieleza kuwa ataendelea kuhudumu katika wadhifa wake wa sasa na kuachia siasa watu wa familia yake.

Kauli yyake inajiri wakati ambapo kuna mabadiliko makubwa ya kisiasa huku familia ya Odinga ikionekana kuendelea kuwa na ushawishi mkubwa katika siasa za taifa.