Makosa ya hijai katika sentensi ambayo huchangiwa mno na shida ya matamshi
MSAMIATI ni jumla ya maneno yanayotumiwa katika lugha fulani.
Msamiati wa lugha huzidi kukua kulingana na mwingiliano wa tamaduni mbalimbali, utohozi wa maneno kutoka lugha ngeni na kuwepo kwa teknolojia mpya.
Msamiati ni muhimu sana katika utunzi wa sentensi. Ili mtu awasilishe ujumbe sharti afahamu maana ya maneno atakayotumia kutunga kila sentensi.
Uteuzi wa msamiati usiofaa katika sentensi hupotosha maana, mkutadha usio sahihi na pia husababisha ukosefu wa uwiano wa kisarufi.
Mojawapo ya changamoto inayosababisha matumizi ya msamiati usiofaa katika sentensi ni kukosa kutofautisha maana ya maneno yanayokaribiana kimatamshi.
Iwapo mtu atakosa kutamka neno ipasavyo na kulitofautisha na jingine kimaana, anaweza kulitumia neno hilo badala ya kitate chake na sentensi yake haitawasilisha maana aliyolenga.
Changamoto hii hujitokeza hasa wanafunzi wasioweza kutofautisha maneno yenye sauti nj na j kimatamshi.
Aghalabu utakumbana na sentesni kama vile: *Magari hayo yamenjaa shehena. *Wageni wale wanakunja kwetu.
*Umeshindanje?
Mifano hii ya sentensi ina maneno yenye silabi za sauti nj na j ambayo yametumiwa visivyo.
Maana ya maneno hayo ni tofauti na maana ambayo mwandishi alikusudia kuwasilisha. Ili kuzisahihisha tunafaa kusema: Magari hayo yamejaa shehena.
Wageni wale wanakuja kwetu. Umeshindaje? Mwanafunzi anayekumbwa na changamoto ya kutofautisha maana ya maneno yanayokaribiana kimatamshi, atumie kamusi kusoma maana ya maneno yanayomkanganya, afanye mazoezi ya kutamka maneno hayo, kuyaandika na kuyatumia katika kutunga sentensi.